Pande hasimu Libya sitisheni uhasama kuwanusuru raia: Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres, amelaani ongezeko la ghasia ndani na katika viunga vya mji mkuu wa Libya ,Tripoli, ambazo zimewaacha raia kadhaa wakipoteza maisha na wengine kujeruhiwa.
Katika taarifa yake iliyotolewa na msemaji wake hii leomjini New York Marekani, Guterres amesema mapigano hayo hususan yanayohusisha uvurumishwaji wa makombora unaofanywa kiholela na makundi yaliyojihami kwa silaha na yanasababisha vifo vingi mkiwemo vya watoto.
Amezikumbusha pande zote husika kuwa matumizi ya nguvu kiholela ni kwenda kinyume na sheria za kibinadamu na za haki za binadamu .
Pia amezihimiza pande zote husika kuruhusu wale walionaswa katika mapigano hayo kupewa misaada ya kibinadamu.
Katibu Mkuu , ametoa wito kwa pande zote katikamzozo kusitisha mara moja mapigano hayo na kuheshimu mkataba wa kusitisha mapigano uliosimamiwa na Umoja wa Mataifa na kamati ya maridhiano.
Amesisitia kuwa mjume wake maalum Ghassan Salame ataendelea kutumia nafasi yake kuendeleza juhudu za kuleta suluhu na kushirikiana na pande zote kufikia muafaka wa kudumu wa kisiasa ambao unakubalika na wote ili kuepusha umwagaji zaidi wa damu na kuwanufaisha watu wa Libya.