Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Okoa mwanao kwa kumnyonyesha miaka 2 mfululizo- WHO

Mama akimnyonyesha mwanae mchanga katika kituo cha afya ya mama na mtoto huko wilaya ya Bumbu, mjini Kinshasa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC.
UNICEF/UN0156352/Dubourthoumieu
Mama akimnyonyesha mwanae mchanga katika kituo cha afya ya mama na mtoto huko wilaya ya Bumbu, mjini Kinshasa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC.

Okoa mwanao kwa kumnyonyesha miaka 2 mfululizo- WHO

Afya

Mtoto anaponyonyeshwa miaka miwili mfululizo bila kupatiwa kimiminika chochote ataepusha gharama kubwa zinazotumika kutibu magonjwa kama vile kuhara, magonjwa ambayo husabaisha na matumizi ya maji yasiyo safi na salama katika kumwandalia maziwa mbadadala badala ya yale ya mama.

 

Hospitali si tu sehemu ya matibabu bali pia ni pahala ambapo panatakiwa kujenga msingi wa afya bora na hivyo kuokoa vifo, amesema Mkurugenzi Mkuu wa shirika la afya ulimwenguni WHO Dkt. Tedros Ghebreyesus kufuatia uzinduzi wa mwongozo mpya wa shirika hilo na lile la kuhudumia watoto, UNICEF wa kuimarisha unyonyeshaji wa watoto.

Mwongozo huo una hatua 10 zinazolenga ngazi ya kisera hospitali na pia huduma yenyewe ya unyonyeshaji ambapo mashirika hayo yanasema ukizingatiwa utaokoa maisha ya watoto 820,000 kila mwaka wenye umri wa chini ya miaka 5.

VIONGOZI WA WHO NA UNICEF WAZUNGUMZIA FAIDA ZA MTOTO KUNYONYA MAZIWA YA MAMA PEKEE

Dkt. Tedros amesema katika hospitali nyingi au jamii yoyote ile iwapo mtoto anaweza kunyonyeshwa maziwa ya mama yake au la kunaweza kuleta tofauti kubwa kati ya kifo na uhai.

Mjini Lilongwe nchini Malawi, mama na mwana ni furaha iliyoje lakin mustakhbali wa mtoto huyu unategemea maziwa ya mama.
© UNICEF/NYHQ2013-1031/Marinovi
Mjini Lilongwe nchini Malawi, mama na mwana ni furaha iliyoje lakin mustakhbali wa mtoto huyu unategemea maziwa ya mama.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa UNICEF Henrietta H. Fore amesema maziwa ya mama ni muhimu kwa afya ya muda mrefu ya mtoto na hupunguza gharama za matibabu ya afya kwani huepusha magonjwa kama vile kuhara.

Hata hivyo viongozi hao wamesema uamuzi wa mama kumnyonyesha mtoto wake kwa miaka miwili mfululizo unahitaji ushirikiano kutoka ngazi ya familia hadi kitaifa.

HATUA 10 KWENYE MWONGOZO HUO

Hatua hizo 10 ni pamoja na hospitali kuweka sera ya unyonyeshaji na kuzingatia kanuni za kimataifa za kuwapatia watoto wachanga maziwa ya kopo iwapo inalazimika kufanya hivyo, na será hizo ziwe bayana kwa wahudumu wa afya.

Halikadhalika hospitali zijadiliane na wajawazito na familia zao kuhusu umuhimu wa kunyonyesha mtoto na pia watoto wachanga wasipatiwe kitu kingine chochote zaidi ya maziwa ya mama labda tu ikiwa kuna tatizo la kitabibu.

Mwongozo pia unataka mama aelekezwe athari za matumizi ya kutumia chupa za kunyweshea mtoto maji au maziwa na hata mpira wa kumwekea mtoto mdomoni ili asilie.