Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IOM na taasisi ya Panzi na usaidizi kwa manusura wa ukatili wa kingono DRC

Wahanga wa ukatili wa kijinsia, nchini DRC. Picha: UM/Marie Frechon

IOM na taasisi ya Panzi na usaidizi kwa manusura wa ukatili wa kingono DRC

Ukiukwaji mkubwa wa haki za wanawake na watoto ikiwemo ukatili wa kingono na utumikishaji watoto kwenye maeneo ya migodi huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC umesababisha Umoja wa Mataifa na wadau wake kuchukua hatua kuepusha zahma zaidi miongoni mwa makundi hayo.

Mmoja wa waathirika wa vitendo hivyo amenukuliwa na shirika la uhamiaji la Umoja wa Mataifa, IOM akisema kuwa analazimika kushiriki ukahaba na wachimbaji wadogo wadogo katika moja ya mgodi  huko jimbo la Kivu Kaskazini ili aweze kuhudumia familia yake ambayo ni watoto wake wanne na mama yake mzazi.

Mwanamke huyo amesema hulipwa dola tatu kwa kila mwanaume anayelazimika kulala naye huku wengine humlipa dola tano kwa usiku mzima jambo ambalo IOM inasema linatokana na mazingira magumu yasababishwayo na vita.

Tayari IOM na taasisi ya Panzi huko Kivu Kusini wanasaka usaidizi ili waweze kutoa huduma za usaidizi kwa manusura wa ukatili wa kingono na kijinsia kwenye eneo hilo lililoko Mashariki mwa DRC.

Usaidizi huo utalenga utoaji wa huduma za matibabu, usaidizi wa kisaikolojia na kuwajumuisha kwenye shughuli za kiuchumi ili waweze kupata kipato.