Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mahakama ya ICC waruhusu kuanza uchunguzi dhidi ya uhalifu nchini Burundi:

Mahakama ya ICC waruhusu kuanza uchunguzi dhidi ya uhalifu nchini Burundi:

Majaji watatu wa mahakama ya kimataifa ya uhalifu ICC leo wameweka hadharani waraka wa kumruhusu mwendesha mashitaka wa mahakama hiyo kuanzisha uchunguzi dhidi ya uhalifu uliotekelezwa Burundi au na raia wa Burundi walioko nje tangu 26 Aprili 2015 hadi 26 Oktoba 2017.

Majaji hao Chang-ho Chung , Antoine Kesia-Mbe Mindua na Raul C. Pangalangan, wamesema mwendesha mashitaka huyo pia anaruhusiwa kupanua wigo wa uchunguzi wake hata kwa makosa yalitotekelezwa kabla ya 26 Aprili 2015 au hata baada ya 26 Oktoba 2017 endapo utakidhi mahitaji ya kisheria yanayohitajika.

Uamuzi huo ulitolewa kwanza kwa siri tarehe 25 Oktoba 2017. Mahakama ilikubali  kuuweka wazi baada ya kumuagiza mwendesha mashitaka kutoa maelezo ya ziada, kufanya kesi kwa siri na kuhakikisha ushiriki wa mwendesha mashitaka tu , ili kuzuia hatari dhidi ya maisha na ustawi wa waathirika na mashahidi.

Majaji wamebaini kwamba mahakama ina mamlaka dhidi ya makosa yaliyofanyika wakati Burundi ilikuwa mwanachama wa mkataba wa Roma hadi ilipojiengua rasmi uanachama 26 Oktoba 2017.

Pia mahakama hiyo ina haki ya kuchunguza makosa hata baada ya Burundi kujiengua endapo makosa yanayochunguzwa yalifanyika wakati nchi hiyo ikiwa bado mwanachama.

Waraka huo pia umeitaka Burundi kutoa ushirikiano kwa mahakama hiyo wakati wa uchunguzi chini ya sheria za mkataba wa Roma.

Kutokana na ushahidi uliopoa miongoni mwa makosa yatakayochunguzwa ni uhalifu dhidi ya ubinadamu ikiwemo mauaji na kujaribu kufanya mauaji, ufungaji watu kiholela na kuwanyima uhuru, mateso, ubakaji, watu kutoweshwa na manyanyaso,  na ni uhalifu uliofanyika ndani ya Burundi au pia kutekeelezwa na raia wa Burundi walioko nje katika kipindi kilichotajwa.