Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Madhila ya raia Mashariki mwa Ghouta Syria yanatia hasira-Zeid

Madhila ya raia Mashariki mwa Ghouta Syria yanatia hasira-Zeid

Hali ya raia takribani 350,000 waliozingirwa katika eneo la Mashariki mwa Ghouta,nje kidogo ya mji mkuu wa Syria Damascus inatia hasira amesema leo Kamisha mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Zeid Ra’ad Al Hussein.

Ametoa wito kwa pande zote katika mzozo kuruhusu msaada unaohitajika haraka wa chakula na madawa kufika katika eneo hilo.

Amesema picha za hivi karibuni za kutisha na kusikitisha zikionyesha watoto walio na utapia mlo wa kupindukia ni ishara ya hali mbaya inayowasibu watu wa Mashariki mwa Ghouta, ambao sasa wanakabiliwa na dharura ya kibinadamu.

Eneo la Mashariki mwa Ghouta limekuwa likizingirwa na vikosi vya serikali kwa zaidi ya miaka minne sasa , na maeneo ya makazi ikiwa ni pamoja na sehemu ambazo awali ziliachwa bila kushambuliwa sasa yamekuwa chini ya mashambulizi karibu kila siku.