Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban aunda jopo kuchunguza madai ya matumizi ya silaha za kemikali Syria

Ban aunda jopo kuchunguza madai ya matumizi ya silaha za kemikali Syria

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ametangaza kuunda jopo la kuchunguza madai ya kuwepo kwa matumizi ya silaha za kemikali nchini Syria.  Bwana Ban amewaeleza waandishi wa habari hii leo kuwa hatua hiyo inafuatia ombi rasmi kutoka mamlaka za Syria la kutaka jopo maalum lisiloegemea upande wowote kuchunguza madai hayo. Katibu Mkuu ametaja kwa muhtasari majukumu ya jopo hilo ambalo kwa sasa amesema washauri wake waandamizi wanashauriana na vyombo kadhaa ikiwemo shirika la kudhibiti silaha za kemikali OPCW na shirika la afya duniani, WHO juu ya vile ambavyo litafanya kazi na uchunguzi utaanza kazi mapema iwezekanavyo.

(SAUTI BAN)

 “Jopo la uchunguzi litaangalia matukio mahsusi ambayo nimeelezwa na Serikali ya Syria. Bila shaka ninatamua kuwa kuna madai mengine kama hayo kuhusu matumizi ya silaha za kemikali. Katika kutekeleza majukumu yake, jopo hilo linahitaji ushirikiano kutoka pande zote. Nasisitiza kuwa hiyo inahusisha kuweza kuingia maeneo yote bila kikwazo. Nitawasiliana na serikali ya Syria kuhusu hilo. Pia nitalijulisha Baraza la Usalama juu ya uamuzi wangu.”

Halikadhalika Bwana Ban amesisitiza kuwa matumizi yoyote ya silaha za kikemikali ni uhalifu dhidi ya binadamu na kwamba Jumuiya ya kimataifa inahitaji hakikisho kamili kuwa malundo ya silaha za kemikali yanathibitishwa na yanahifadhiwa kwa usalama.