UNHCR yahitaji msaada wa dharura wa zaidi ya milioni 83 kusaidia Warohingya
Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR, limetangaza ombi la msaada wa dharura wa dola milioni 83.7 kwa ajili ya kusaidia mahitaji ya kiusalama kwa wakimbizi zaidi ya laki 5 wa rohingya walioko nchini Bangladesh.
Msemaji wa UNHCR Andrej Mahecic amesema, msaada huo wa dharura utakaoelekezwa kwenye kambi za Kutupalong na Nyapara, utalenga ulinzi wa wakimbizi, makazi, maji na usafi wa mazingira na pia kuimarisha uwezo wa wenyeji wa kusini-mashariki mwa Bangladesh ambao wanasaidia wakimbizi hao.
Ameongeza kuwa idadi kubwa ya wakimbizi ni wanawake, wazee na watoto ambao wengi wao hawajaambatana na familia zao au wametengana na familia zao.
Hata hivyo UNHCR imesema ingawa bado pesa zinahitajika kukidhi mahitaji ya dharura ya mwezi septemba 2017 hadi Februari ya 2018, wanachukua fursa kushukuru mashirika ya misaada na serikali ambazo tayari zimesaidia.