Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mfumo wa mahakama Burundi hauko huru- Ripoti

Mfumo wa mahakama Burundi hauko huru- Ripoti

Kamisheni iliyoundwa kuchunguza ukiukwaji wa haki za binadamu nchini Burundi umebaini kuwa mfumo wa mahakama nchini humo hauko huru hasa baada ya mwezi Aprili mwaka 2015, mahakama iliporuhusu Rais Pierre Nkurunzinza kuwania urais kwa awamu ya tatu.

Wakiwasilisha ripoti yake mbele ya Baraza la Haki za binadamu la Umoja wa Mataifa huko Geneva, Uswisi  hii leo , wajumbe wa kamisheni hiyo wamesema hilo hi dhahiri na katika mazingira hayo ukwepaji sheria umetamalaki hasa miongoni mwa maafisa wa usalama wa Taifa na wanachama wa chama tawala huku ukiukwaji wa haki za binadamu  ukiendelea pasi hatua zozote kuchukuliwa.

Ni kwa mantiki hiyo kamisheni ya uchunguzi inaamini pengine serikali haina nia au haiwezi kufanya uchunguzi wa kina na kufungua mashtaka dhidi ya watekelezaji wa vitendo vya ukiukwaji wa haki.

Kamisheni hiyo ya uchunguzi imependekeza mambo kadhaa ikiwemo watuhumiwa wa ukiukaji wa haki za binadamu wasiruhusiwe kushiriki kwenye operesheni za ulinzi wa amani za Umoja wa Mataifa au Muungano wa Afrika.