Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Viongozi Kenya tumeni ujumbe wa wazi kwa wafuasi kuepusha vurugu- Guterres

Viongozi Kenya tumeni ujumbe wa wazi kwa wafuasi kuepusha vurugu- Guterres

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres amepongeza watu wa Kenya kwa kushiriki uchaguzi mkuu kwa amani.

Kwa mujibu wa taarifa ya msemaji wake, Guterres amesikia matokeo na hatimaye  Uhuru Kenyatta kutangazwa na Tume huru ya uchaguzi na mipaka IEBC kuwa rais mteule.

Hata hivyo Bwana Guterres ametoa wito kwa viongozi wa kisiasa wanaopinga matokeo ya uchaguzi kuelekeza malalamiko yao kupitia vyombo vinavyokubalika kisheria.

Aidha ametoa wito kwa viongozi wa kisiasa watume ujumbe ulio wazi kwa wafuasi wao wa kuwahimiza wajiepushe na vurugu huku akisisitiza umuhimu wa majadiliano katika kuzuia uhasama.

Amesema Umoja wa Mataifa, kwa ushirikiano na Muungano wa Afrika na wadau, unashirikiana na mamlaka za kisiasa na washikadau ili kufanikisha kukamilika kwa mchakato wa uchaguzi kwa njia fanisi.