Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kutatua zahma ya wakimbizi Uganda vita lazima viishe Sudan Kusini:Guterres

Kutatua zahma ya wakimbizi Uganda vita lazima viishe Sudan Kusini:Guterres

Suluhu ya wimbi kubwa la wakimbizi barani Afrika tangu mauaji ya Kimbari ya Rwanda ni kumaliza mgogoro wa Sudan Kusini amesema leo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres . John Kibego na taarifa kamili

(TAARIFA YA KIBEGO)

António Guterres ameyasema hayo katika hotuba yake kwenye siku ya pili ya mkutano wa kimataifa wa mshikamano na wakimbizi unaofanyika mjini Kampala , Uganda.

Idadi ya watu walioomba hifadhi kwenye taifa hilo la Afrika ya Mashariki imekuwa zaidi ya mara mbili katika mwaka mmoja uliopita na kufikia zaidi ya milioni 1.2.

Katika hotuba yake Guterres ameishukuru serikali na watu wa Uganda kwa kuonyesha utu dhidi ya wakimbizi kwa kuwapokea na kuwahifadhi hata hivyo amehimiza kuwa suluhu ya kudumu ya mgogoro wa Sudan Kusini ni muhimu

(SAUTI YA SG)

“Tunaamini kwamba hitimisho la kwanza ni lazima, kila kitu lazima kifanyike kuhakikisha vita vya Sudan Kusini vinamalizwa. Na nataka kushukuru juhudi zako rais Yoweri Museveni, unazofanya ili kuweka mazingira ambayo awali watu walioungana kwa ukombozi wa nchi yao, waweze kurejea tena kwenye umoja na kuleta amani nchini mwao"

Wakuu wa nchimbalimbali wamehudhuria mkutano huo ikiwemo , Gabon, Zambia, Somalia na Equatorial Guinea, na makamu wa Rais wa Burundi na Sudan Kusini.

Uganda inahifadhi wakimbizi 900,000 kutoka Sudan Kusini na 400,000 kutoka Burundi kwa mujibu wa shirika la wakimbizi UNHCR.