Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wakati umewadia kutokomeza Fistula kila kona ya dunia: Babatunde

Wakati umewadia kutokomeza Fistula kila kona ya dunia: Babatunde

Matumaini, uponyaji na utu kwa wote ni ndio kauli mbiu ya mwaka huu ya siku ya kimataifa ya kutokomeza Fistula, hiyvo jumuiya ya kimataifa inatakiwa kushikamana na kujitolea kuhakikisha maisha ya wanawake na wasichana walioathirika na Fistula yanabadilina na jinamizi hilo linatokomezwa kabisa.

Wito huo umetolewa na mkurugenzi mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la idadi ya watu duniani UNFPA Dr. Bababtunde Osotimehin katika ujumbe maalumu wa siku hii ambayo kila mwaka huadhimishwa Mei 23.

Amesisitiza kuwa ni muhimu kuhakikisha haki za msingi za binadamu kwa wanawake na wasicha zinazingatiwa kila pembe ya dunia hasa kwa wale walioachwa nyuma, kutengwa na kupuuzwa katika jamii kutokana na Fistula.

Dr. Osotimehin amesisitiza kuwa kutokomeza Fistula ni kipaumbele cha UNFPA na ni hatua muhimu katika kuelekea utimizaji wa ajenda ya maendeleo endelevu ya 2030. Fistula imeshatokomezwa katika nchi tajiri hivyo inawezekana ameongeza na sasa inaweza kutokomezwa katika nchi masikini kwa kuwa na mifumo imara ya afya na kushughulikia masuala yanayosababisha tatizo hilo ikiwemo usawa wa kijinsia, kukomesha ndoa za mapema, kujifungua katika umri mdogo,na ukosefu wa elimu.

Zaidi ya wanawake na wasichana milioni mbili bado wanaishi na Fistula na wengine kati ya 50,000 na 100,000 wanapata fistula kila mwaka.