Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ofisi ya haki za binadamu yalaani ukatili Sudan Kusini; yataka uwajibikaji kisheria

Ofisi ya haki za binadamu yalaani ukatili Sudan Kusini; yataka uwajibikaji kisheria

Ofisi ya haki za binadamu katika Umoja wa Mataifa (OHCHR) imelaani machafuko yaliyoibuka karibuni katika miji kadhaa ya Sudan Kusini, ikwemo Pajok katika jimbo la Equatoria Mashariki na Wau katika Bahr el-Ghazal, ambayo yamesababisha vifo vingi vya raia na kuwalazimu zaidi ya watu 22,000 kuhama makwao.

Machafuko hayo yalifuatia mashambulizi ya kuviziwa dhidi ya wanajeshi wa serikali (SPLA) na watu wenye silaha, ambapo wanajeshi hao walijibu kwa kuanza kuwashambulia raia kiholela.

Taarifa ya ofisi hiyo imesema kuwa maafisa wake walipoyazuru maeneo hayo, walipata ripoti za ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu, yakiwemo mauaji holela ya raia, ukatili wa kingono, uporaji na uharibifu wa mali za raia, na ukwepaji sheria ulioenea kwa ukiukaji huo.

Ravina Shamdasani ni msemaji wa Ofisi ya haki za binadamu, Geneva.

"Kuenea kwa ukwepaji sheria kwa mashambulizi katili dhidi ya raia kunachochea tu ukatili zaidi. Tunatoa wito kwa mamlaka zihakikishe kuwa wanaowajibika kwa ukatili wa Pajok na Wau wanakabiliwa kisheria, bila kujali wanakoegemea kisiasa au nyadhfa zao.”