Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuna haja ya kuimarisha mifumo ya afya kukabiliana na dharura za kiafya- Ban

Kuna haja ya kuimarisha mifumo ya afya kukabiliana na dharura za kiafya- Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, amesema ripoti zilizochapishwa na jopo la ngazi ya juu kuhusu jitihada za kimataifa wakati wa mizozo ya kiafya, zinabainisha moja ya changamoto za dharura na za muda mrefu zaidi katika nyakati za sasa.

Ban amesema, mnamo mwezi Februari mwaka huu, jopo hilo lilichapisha ripoti iliyotoa mapendekezo 27 ya hatua za kuchukua kwenye ngazi za kitaifa, kikanda, na kimataifa.

Jopo hilo lilisisitiza kuwa kuifanya mifumo ya afya iwe imara zaidi na tayari kwa dharura kunahitaji utafiti na maendeleo vumbuzi, ufadhili tosha, na uungwaji mkono kupitia mipango ya maendeleo.

image
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon akihutubia kikao cha leo.(Picha:UM/Eskinder Debebe)
 “Jopo hilo lilipendekeza kuwa uwezo wa WHO wa kushughulikia dharura za kiafya ni lazima uratibiwe vyema na kuimarishwa. Pili, jopo lilipendekeza umuhimu wa kuimarisha mfumo wa Umoja wa Mataifa wakati wa mizozo ya kiafya, na kukariri jukumu muhimu la kamati ya dharura inayojumuisha mashirika mbalimbali ya Umoja huo.

Akizungumza kwa njia ya video kutoka jijini Dakar, Senegal, mwenyekiti wa jopo hilo ambaye ni Rais Mstaafu wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, amesema jopo hilo lilibaini kuwa mlipuko wa Ebola uliweka dhahiri udhaifu mkubwa katika mfumo wa kimataifa wa afya.

image
Mwenyekiti wa jopo hilo ambaye ni Rais Mstaafu wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete.(Picha:UM/Eskinder Debebe)
“Ni mtazamo wa jopo kwamba, udhaifu huu usiposhughulikiwa ipasavyo, ukitokea tena mlipuko wa Ebola, hali huenda ikawa mbaya zaidi, na huenda ikawa hata mbaya zaidi iwapo kutakuwa na mlipuko wa maradhi yanayoambukiza kupitia hewani.”

Aidha amesema jopo hilo lilibaini kuwa mifumo ya afya katika nchi zenye maendeleo duni ni dhaifu.

“Kwa hiyo nchi hizo zinakabiliwa na hatari iwapo kutakuwa na milipuko ya magonjwa, kwa sababu zina uwezo mdogo wa kuizuia au kuishughulikia. Hili lilidhihirishwa Liberia, Guinea na Sierra Leone.”