Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la usalama laridhia kuundwa kwa JIM, Ban azungumza

Baraza la usalama laridhia kuundwa kwa JIM, Ban azungumza

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amekaribisha hatua ya Baraza la usalama kupitisha siku ya Alhamisi, azimio la kuridhia pendekezo lake la kuunda na kuendesha chombo cha pamoja cha uchunguzi na shirika la kimataifa la kupinga silaha za kemikali, OPCW.

Taarifa ya msemaji wa Umoja wa Mataifa imemnukuu Ban akisema kuwa hatua hiyo ya kuunda JIM, inawekea msisitizo suala la kushughulikia matumizi ya kemikali za sumu kama silaha na umuhimu wa watumiaji wa kemikali hizo kuwajibishwa.

Taarifa imeongeza kuwa bila kuchelewa, Katibu Mkuu kwa uratibu wa karibu na Mkurugenzi Mkuu wa OPCW na wadau wengine husika watachukua hatua zote na mipango ya lazima ili kuunda chombo hicho na kianze kazi haraka.

Bwana Ban amesisitiza wito wake kwa pande zote husika huko Syria kushirikiana vyema na chombo hicho akisema anaendelea kuweka matumaini  yake kwa ushiriki na kuungwa mkono na Baraza la usalama na Umoja wa Mataifa kuhakikisha azimio hilo linatekelezwa.