Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kupambana na utipwatipwa ni wajibu wa jamii: WHO

Kupambana na utipwatipwa ni wajibu wa jamii: WHO

Shirika la Afya Duniani WHO limezindua leo ripoti yake ya muda kuhusu kusitisha utipwatipwa wa watoto ikisema idadi ya watoto wanaokumbwa na unene huo wa kupindukia imeongezeka kwa asilimia 47 tangu mwaka 1980, hasa kwenye nchi zenye kipato cha juu.

Kwa mujibu wa WHO mweleko huo unaanza kuongezeka pia kwenye nchi zinazoendelea.

Ripoti hiyo iliyoandaliwa na kamisheni maalum kuhusu suala hilo,inaeleza kwamba utipwatipwa si kosa la watoto bali hutokana na mazingira wanamoishi ambayo yanawashawishi kula vyakula venye sukari na mafuta zaidi bila kusahau vyakula walivyopatiwa wakiwa wadogo au hata kabla ya kuzaliwa.

Kwa hiyo, ripoti inasema, ni wajibu wa jamii kupunguza hatari za utipwatipwa kwa watoto, afya ya mtoto ikiwa ni moja ya haki zake za msingi.

Miongoni mwa mapendekezo ya ripoti hiyo ni kuelimisha watoto shuleni kuhusu lishe nzuri kwa afya, kusaidia shule kwenye maeneo yenye kipato cha chini kuwapatia watoto milo mizuri kwa afya au kuweka kiwango cha juu cha ushuru juu ya vinyaji venye sukari.

Aidha WHO imeeleza kuwa ni muhimu kuwezesha watoto na wanafunzi kufanya mazoezi ya kutosha. huku ripoti ikimulika umuhimu wa kuelimisha wanawake wajawazito kuhusu umuhimu wa unyonyeshaji na lishe bora kwa watoto.