Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nafasi ya demokrasia Myanmar yadidimia katika mwaka wa uchaguzi- Mtaalam wa UM

Nafasi ya demokrasia Myanmar yadidimia katika mwaka wa uchaguzi- Mtaalam wa UM

Mtaalam maalum wa haki za binadamu katika Umoja wa Mataifa amesema kuwa hatua zilizokuwa zimepigwa katika kuendeleza uhuru wa kujieleza na kufanya mikutano nchini Myanmar zimo hatarini kudidimia.

Mtaalam huyo, Yanghee Lee amesema hayo wakati akihitimisha ziara yake ya siku kumi nchini Myanmar, akiongeza kuwa kuna ishara kwamba tangu alipoizuru nchi hiyo awali, vizuizi kwa shughuli za mashirika ya umma na vyombo vya habari vimeongezeka.

Bi Lee ameelezea wasiwasi wake kuhusu kuhangaishwa na vitisho kwa waandishi wa habari na wanaharakati wa umma na waandamanaji wanaoipinga miradi ya serikali au kutetea uwajibikaji wa maafisa wa serikali, akitoa mfano wa visa vya hivi karibuni ambapo nguvu zilitumiwa kupita kiasi dhidi ya wakulima wa vijijini na wakazi wa mjini waliokuwa wakiandamana dhidi ya miradi fulani ya maendeleo.

Amesema iwapo Myanmar kweli inataka kubadilika na kuelekea demokrasia, ni lazima iwaruhusu watu wanaoathiriwa na shughuli za serikali wajieleze kuhusu kinachowaudhi bila kuadhibiwa.