Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uamuzi mgumu ufanyike kuokoa wakimbizi wa Syria na Iraq: UNHRC

UNHCR yaonya kuhusu mzozo wa msimu wa baridi nchini Syria.(Picha ya UNHCR)

Uamuzi mgumu ufanyike kuokoa wakimbizi wa Syria na Iraq: UNHRC

Huko Mashariki ya kati, Mratibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la wakimbizi UNHCR nchini Syria Amin Awad ameonya kuwa ni lazima uamuzi mgumu ufanyike katika kuwanusuru wakimbizi wa Syria na Iraq waliokimbia makwao kutokana na machafuko wakati huu ambapo msimu wa baridi kali unakaribia. Taarifa kamili na Grace Kaneiya(TAARIFA YA GRACE)

Akiongea katika mkutano na waandishi wa habari mjini Geneva Bwana Awad amesema kuwa UNHCR linalazimika kutoa kipaumbele kusaidia wakimbizi hao hususani katika muundo wa makambi ambayo yatakabiliana na baridi kali.

Amesema kuwa shirika hilo kadhalika linajielekeza katika kundi hatarishi zaidi la watoto wachanga na, wazee na wagonjwa watakaokumbana na hali hiyo ya hewa ikiwamo theluji, upepo mkali na mvua akiongeza kuwa idadi ya wakimbizi wa ndani imeongezeka kufikia zaidi ya milioni 13 katika nchi hizo mbili. Bwana Awad amesema kiasi cha dola milioni 58 kinahitajika ili kuwasaidia wahitaji hao.

(SAUTI YA AWAD)

"Natamani kama tungeweza kutoa msaada kwa kila mtu na iwapo tungeweza kumkinga kila mtu dhidi ya baridi. Lakini ukweli ni kwamba wakazi wanahama na wanaendelea kuhama hadi mwishoni mwa mwaka huu, na kiasi  cha fedha tunachopokea kinakuja pole pole, na sasa tumeingia wiki ya pili mwezi Novemba na msimu wa baridi umewadia . Kwa hivyo inatulazimu tuweke vipaumblele na tuchukue uamuzi mgumu lakini bado tunatamani tungalikuwa na fedha hizo leo."