Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mauritania badili ahadi kuwa vitendo ili kudhibiti utumwa: Mtaalamu

Mauritania badili ahadi kuwa vitendo ili kudhibiti utumwa: Mtaalamu

Mtaalamu maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu utumwa Gulnara Shahinian amepongeza Mauritania kwa hatua ilizochukua kutokomeza utumwa nchini humo lakini akataka vitendo zaidi kwa kutekeleza sheria na sera.

Amesema hayo mwishoni mwa ziara yake rasmi nchini humo ya kutathmini utekelezaji wa mapendekezo ya awali ambapo ametaja hatua hizo kuwa ni pamoja na mpango wa kuanzisha mahakama maalum ya makosa kuhusu utumwa na sheria inayoharamisha kitendo hicho.

Hata hivyo Bi. Shahinian amesema vitendo zaidi vyahitajika kutekeleza sera na sheria na kuangalia upya makosa dhidi ya utumwa kwenye sheria husika kwani inaangua baadhi ya waathirika.

Akiwa nchini humo kwa siku nne alikutana na viongozi wa serikali, mashirika ya kimataifa na yale ya kiraia bila kusahau vyama vya wafanyakazi na watu wanaojihusisha na vita dhidi ya utumwa.

Amesema vikundi vya kiraia vina dhima kubwa katika kutokomeza utumwa kwa kuhamasisha jamii kuelewa aina ya utumwa na mbinu za kuondokana nao.

Mtaalamu huyo maalum atawasilisha ripoti ya ziara yake Mauritania kwenye kikao kijacho cha Baraza la haki za binadamu mwezi Septemba mwaka huu.