Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNDP yaanzisha mpango wa kuijenga upya CAR

UNDP yaanzisha mpango wa kuijenga upya CAR

Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa UNDP,limezindua mpango unaogharimu dola za Marekani milioni 26 kwa ajili ya kuendeleza majukumu ya ujenzi wa amani katika taifa la Jamhuri ya Kati.George Njogopa na taarifa kamili.

(Taarifa ya George)

Mpango huo wa miaka miwili ulizinduliwa leo mjini Bangui unashabaha ya kujenga jamii yenye maridhiano na kufufua matumaini mapya kwa wananchi walioathiriwa na mapigano yaliyolikumba taifa hilo katika kipindi cha kuanzia mwaka uliopita.

Zaidi ya watu 350,000 wanatazamiwa kufikiwa na mpango huo ambao pia utahakikisha unarejesha katika hali yake ya kawaida baadhi ya miundo mbinu iliyoharibiwa na machafuko hayo ya kisiasa ambayo baadaye yalichukua sura ya kidini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango huo, mwakilishi mkazi wa UNDP  Kaarina Immonen alisema kuwa shabaha kubwa ni kuona kwamba daraja jipya la matumaini linajengwa kwa watu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati na kwamba maeneo yatayozingatiwa ni yale yanayohusu masuala ya kiuchumi, kijamii nay ale yanayohusu usalama jumla

Inaarifiwa kuwa zaidi ya nusu ya wananchi wa taifa hilo wanahitaji msaada wa dharura kutokana na uharibufu mkubwa uliosababishwa na machafuko yanayoendelea.