Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkuu wa OCHA kuzuru Ufilipino kujionea hali halisi

Mkuu wa OCHA kuzuru Ufilipino kujionea hali halisi

Mkuu wa masuala ya usaidizi wa binadamu kwenye Umoja wa Mataifa Bi. Valerie Amos Jumatano hii anaanza ziara ya siku Mbili nchini Ufilipino kutathmini hali ya usaidizi wa kibinadamu takribani miezi minne baada ya kimbunga Haiyan kupiga nchi hiyo na kuathiri watu Milioni 14.

Taarifa ya OCHA shirika analoongoza Bi. Amos imesema wakati wa ziara hiyo atakuwa na mazungumzo na viongozi wa serikali, mamlaka za maeneo yaliyokumbwa na kimbunga hicho na wadau katika misaada ya kibinadamu.

Halikadhalika atakwenda Guiuan na Tacloban kukutana na wahanga wa kimbunga hicho.

Habari zinasema wakati operesheni za usaidizi zinazoongozwa na serikali zikiendelea, mamilioni ya watu bado wanahitaji misaada ya dharura kujenga upya maisha yao wakati huu ambapo zaidi ya nyumba Milioni Moja zimeharibiwa na zaidi ya watu Milioni Nne hawana makazi. Shughuli za kiuchumi kama vile kilimo na uvuvi nazo zimekwama na hivyo kusababisha mkwamo kwa uwezo wa watu kuendesha maisha yao.

Hii itakuwa mara ya pili kwa Bi. Amos kutembelea Ufilipino baada ya janga la Haiyan, ambapo mara ya mwisho ilikuwa Novemba 2013.