Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IOM yatoa msaada wa dharura kwa wakimbizi wa ndani Malakal Sudan Kusini

IOM yatoa msaada wa dharura kwa wakimbizi wa ndani Malakal Sudan Kusini

Mapigano makubwa mjini Malakal makao  makuu ya jimbo la Upper Nile Sudan Kusini yamesababisha uharibifu na kutawanya maelfu ya watu waliolazimika kuzikimbia nyumba zao zaidi ya mwezi mmoja uliopita, huku ikikadiriwa kuwa watu 27,000 wamechukua hifadhi katika ogisi za mpango wa Umoja wa mataifa UNMISS mjini Malakal. Flora Nducha na taarifa kamili

(TAARIFA YA FLORA NDUCHA)

Kwa sasa shirika la kimataifa la uhamiaji IOM liko msitari wa mbele kuwasaidia maelfu ya wakimbizi wa ndani walioko Malakal na maeneo mengine ya Sudan Kusini.

IOM inawapa msaada wa vifaa vya malazi na visivyo chakula, vifaa vya afya na maji na huduma ya usafi, ikiwa ni pamoja na kuwaorodhesha watu ili waweze kupatiwa msaada huo.

Kwa mujibu wa shirika hilo hali ya usalama mdogo Malakal imetoa changamoto ya kufikisha misaada ya kutosha hasa malori yaliyo na majisafiya kunywa. Changamoto nyingine ni msongamano wa watu katika eneo la UNMISS ambalo awali lilikuwa ni kwa ajili ya wafanyakazi tuu.

IOM inashirikiana na wadau wengune wa misaada ya kibinadamu ili kuwalinda wakimbizi hao na kuhakikisha kwamba kuna nafasi ya kutosha kujenga huduma muhimu kama vyoo na visima vya maji.