Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mashirika ya Umoja wa Mataifa kuongeza juhudi kukabili mzozo wa Syria:UNDP

Mashirika ya Umoja wa Mataifa kuongeza juhudi kukabili mzozo wa Syria:UNDP

Wakurugenzi na wawakilishi wa mashirika 22 ya Umoja wa mataifa wameafikiana kuzindua mpango wa pamoja wa maendeleo kwa ajili ya kukabili mzozo wa Syria  kwenda sambamba na juhudi za kibinadamu zinazoendelea za kutoa misaada ya kuokoa maisha kwa wakimbizi wa ndani ya Syria na katika nchi jirani.

Muafaka huo umepatikana katika mwisho wa mkutano wa zaidi ya siku mbili uliohusisha wakurugenzi wa kikanda na mashirika ya Umoja wa Mataifa.

Sima Bahous ambaye ni naibu katibu mkuu, mwenyekiti kundi la maendeleo la kikanda la Umoja wa mataifa UNDG na mkurugenzi wa ofisi ya kanda kwa mataifa ya Kiarabu kwenye shirika la maendeleo la Umoja wa mataifa UNDP aliyeitisha mkutano huo ametaka sio tuu kupanua wigo wa shughuli za Umoja wa Mataifa lakini pia kubadili mwelekeo wa juhudi hizo.

Amesema wakati wanaendelea kutoa misaada ya kibinadamu ni lazima pia washughulikie mahitaji ya kimaendeleo kwa njia ambayo inasaidia na ya haraka. Ameongeza kuwa ni lazima kulinda hatua za maendeleo zilizopo lakini pia kuimarisha ujenzi mpya ili watu wanaosaidiwa waweze kukabili machafuko yanayoendelea na kujenga upya maisha yao.