Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Sitisheni mapigano Syria ili raia waelekee maeneo salama: Mkuu wa OCHA

Sitisheni mapigano Syria ili raia waelekee maeneo salama: Mkuu wa OCHA

Mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa inayoratibu misaada ya kibinadamu Valerie Amos ametaka kuwepo kwa makubaliano ya kusitisha mapigano huko Moadamiyeh nchini Syria ili kutoa fursa kwa raia walionasa kwenye mazingira ya mzozo waweze kuhamia maeneo salama. Taarifa iliyotolewa na ofisi ya msemaji wa Umoja wa Mataifa Jumamosi imemkakari Bi. Amos akielezea wasiwasi wake mkubwa juu ya kile kinachoendelea eneo hilo  na maeneo mengine ya Syria ambako wanawake na watoto pamoja na wanaume wanakumbwa na ghasia kutoka pande mbili zinazokinzana nchini humo. Amesema kwa miezi kadhaa sasa wameshindwa kuingia eneo la Moadamiyeh huko Damascus na kwamba licha ya wananchi Elfu Tatu kuhamishwa Jumapili iliyopita, bado idadi kama hiyo wamenasa. Amesema walionasuliwa tayari wanapata misaada kutoka chama cha msalaba mwekundu nchini Syria pamoja na Umoja wa mataifa na wadau wake. Amesema wanapaswa kuwezeshwa kuhamia maeneo salama bila hofu ya kuweza kushambuliwa. Mkuu huyo wa OCHA ametaka pande zote zinazozozana Syria ziheshimu sharia za kimataifa kuhusu binadamu na wawezeshe watoa usaidizi wa kibinamu kuwafikia wananchi popote pale walipo nchini humo.