Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uhaba wa vyoo wasababisha utoro wa watoto wa kike shuleni: UNICEF

Uhaba wa vyoo wasababisha utoro wa watoto wa kike shuleni: UNICEF

Katika kuelekea siku ya mtoto wa kike duniani  hapo kesho, nchini Bangladesh, ubunifu wa mbinu rahisi na salama umewezesha kurejesha watoto wa kike shuleni ambao awali waliamua kuacha masomo kutokana na  uhaba wa vifaa vya kujisafji pamoja na vyoo. Deepti Rani Devi ambaye ni Mwalimu katika shule hiyo iitwayo Shahid Shudorshon amesema mwaka 2011 walishuhudia utoro miongoni mwa wanafunzi wa kike kuwa karibu asilimia 50. Walifanya utafiti na kubaini kuwa watoto wa kike walishindwa kuhudhuria masomo kutokana na uhaba wa vyoo, kwa kuwa shule yao ilikuwa na vyoo viwili tu kwa wanafunzi 1,400 na hivyo walishindwa kujisafi ipasavyo. Hata hivyo kwa ushirikiano kati ya mamlaka za serikali za mitaa na shirika la Umoja wa mataifa la kuhudumia watoto, waliweza kuchangisha fedha na kujenga vyoo 18 shuleni hapo pamoja na kuweka vifaa vya kujisafi.

Mwalimu Devi amesema hivi sasa mahudhurio ya watoto wa kike yamebadilika ambapo asilimia 66 ni watoto wa kike.