Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nchi za Ulaya zingatieni haki za binadamu kwa wahamiaji: wataalamu UM

Nchi za Ulaya zingatieni haki za binadamu kwa wahamiaji: wataalamu UM

Mtaalamu wa umoja wa Mataifa kuhusu haki za wahamiaji, François Crépeau, amerejelea tena wito wake kwa nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya kuangalia upya mtazamo wao kwa wahamiaji na kuhakikisha unazingatia haki za binadamu. Bwana Crépeau akizungumza mjini New York baada ya kukamilika kwa mjadala wa ngazi ya juu kuhusu uhamiaji na maendeleo amesema tukio la Lampedusa linadhihirisha janga la kibinadamu linavyoweza kusababishwa na mambo ya uhamiaji.

 Ni wahamiaji 150 tu kati ya 500 waliokuwemo kwenye boti hiyo ndio walioweza kuokolewa. Amesema iwapo uhamiaji bila vibali utaendelea kuwa ni tukio la kihalifu bila kuangalia upya sheria za uhamiaji hususan kwa wafanyakazi wenye stadi za chini, basi idadi ya wahamiaji wanaoweka rehani maisha yao ili wafike Ulaya itazidi kuongezeka.

Naye mtaalamu huru wa Umoja wa Mataifa kuhusu Somali, Shamsul Bari na yule wa Eritrea Sheila B. Keetharuth wamesema tukio la Lampedusa inaonyesha kukata tamaa kunakokumba wakazi wa maeneo kama vile Somalia kutokana na ukosefu wa usalama na uchumi uliodumaa.