Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kundi la Séléka lazidi kudidimiza haki za watoto: Zerrougui

Kundi la Séléka lazidi kudidimiza haki za watoto: Zerrougui

Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa watoto walionaswa katika maeneo ya mizozo Leila Zerrougui ameonyesha wasiwasi wake juu ya vitendo vya ukiukwaji wa haki za watogo vinavyofanywa na vikundi vyenye silaha vya kundi la Séléka huko Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Katika taarifa yake amesema kumekuwepo na ripoti kuwa takribani katika kila mji unaodhibitiwa na Séléka , watoto wanaandikishwa jeshini ambapo wavulana wakiwa wamevalia sare za kijeshi na silaha wameonekana wakifanya doria maeneo mbali mbali ya nchi hiyo.

Bi. Zerrougui amesema ukosefu wa utawala wa kisheria pamoja na usalama vinaweka mazingira kwa watoto kuandikishwa upya kwenye vikosi na ametaka makamanda wote husika na vikosi hivyo kuwaachia watoto mara moja.

Mwakilishi huyo maalum pia ametaka uongozi wa Séléka na mamlaka mpya ya mpito nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati kutumia ushawishi wao kutokomeza vitendo vya ukiukwaji wa haki za watoto na wakiukaji wa sheria wachukuliwe hatua.