Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali ya kibinadamu nchini Syria yazidi kuzorota

Hali ya kibinadamu nchini Syria yazidi kuzorota

Shirika la mpango wa chakula duniani, WFP limesema hali ya kibinadamu nchini Syria inazidi kuzorota ambapo mahitaji ya chakula yanazidi kuongezeka, halikadhalika idadi ya watu wanaopoteza makazi yao.

Msemaji wa WFP Elizabeth Byrs amewaambia waandishi wa habari mjini Geneva, Uswisi kuwa hivi sasa wanahudumia watu Milioni Moja na Nusu kwa mwezi nchini Syria. Hata hivyo kuendelea kusambaa kwa mapigano kunasababisha washindwe kufikia maeneo kama vile yale ya kaskazini. Amesema katika maeneo ya mapigano, bei za vyakula zimeongezeka maradufu.

Wakati huo huo shirika la afya duniani WHO limesema hali ya utoaji wa huduma ya afya inazidi kudorora kwa kuwa wagonjwa na watoa huduma wanashinda kufika vituo vya afya kwa sababu ya hofu ya usalama.