Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wataalamu wa UM waonyesha wasiwasi juu ya rasimu ya Katiba Misri

Wataalamu wa UM waonyesha wasiwasi juu ya rasimu ya Katiba Misri

Jopo la wataalamu huru wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa limeonyesha wasiwasi kuhusu mwelekeo wa rasimu ya katiba nchini Misri na kuitaka serikali ya nchi hiyo kuhakikisha mwishowe Katiba inakuwa si ya kibaguzi bali inalinda usawa na kuendeleza haki za wanawake.

Mmoja wa wataalamu hao Kamala Chandrakirana amesema mpaka sasa fursa muhimu ya kipindi cha mpito haijaweza kutumika ipasavyo nchini Misri.

Taarifa ya Ofisi ya Haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa imemkariri Bi. Chandrikana akisema akisema kuwa kipindi cha mpito wa kisiasa kwa kawaida hutoa fursa ya kubadili mifumo ya kibaguzi na kuweka mifumo bora, lakini kipindi hicho kisipotumika vizuri kinaweza kuweka mifumo mingine ya kibaguzi.

Ametolea mfano kikundi kilichoandaa rasimu ya katiba ambacho amesema hakikuwa na mjumbe mwanamke hata mmoja.

Amesema kwa kuzingatia mazingira hayo, masuala ya wanawake hayakuweza kuwasilishwa rasmi kwenye rasimu hiyo.

Rasimu ya mwisho ya katiba mpya ya Misri iliyopitishwa na Bunge la nchi hiyo tarehe 30 mwezi uliopita inatarajiwa kupigiwa kura ya maoni hapo kesho Jumamosi.