Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkurugenzi mkuu wa UNESCO alaani uharibifu kwenye maeneo ya kale nchini Syria

Mkurugenzi mkuu wa UNESCO alaani uharibifu kwenye maeneo ya kale nchini Syria

Mkurugenzi mkuu wa shirika la elimu, sayansi na utamaduni la Umoja wa Mataifa UNESCO Irina Bokova hii leo ameelezea wasi wasi wake kutokana na ghasia zinazoendelea nchini Syria hasa zile zinazolenga sehemu za kitamaduni nchini humo.

Bokova pia anarejelea wito wake alioutoa tarehe 30 mwezi machi mwaka huu wa kuzitaka pande husika kulinda itikadi na tamaduni nchini Syria.Matamshi ya Bi Bokova yanajiri baada ya ripoti za uharibifu wa musikiti wa Umayyad mjini Aleppo uliofanyika wakati wa mapigano makali ya kuudhibiti mji huo.

Bokova amesema kuwa amesumbuliwa na habari za kila siku za kuteseka kwa watu na uharibifu wa maeneo ya utamaduni kote chini. Bokova ameongeza kuwa wanaohusika watafikishwa mbele ya sheria sio tu kwa kupotea kwa maisha ya watu bali pia kwa uharibifu wa sehemu za kale.