Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IAEA yapongeza maandalizi ya Belarus kutumia nyuklia

IAEA yapongeza maandalizi ya Belarus kutumia nyuklia

Shirika la Umoja wa Mataifa la nishati ya atomiki, IAEA limesema Belarus imepiga hatua kubwa katika kuandaa miundombinu ya nyuklia na kuongeza kuwa iwapo itaendelea hivyo basi itaweza kujenga mtambo wa nyuklia siku za usoni.

Hayo yamo katika ripoti ya shirika hilo ambayo Naibu Mkurugenzi Mkuu wake Alexander Bychkov ameikabidhi kwa Naibu Waziri Mkuu wa Belarus Anatoly Tozik, nchi ambayo imeazimia kuwa na mitambo miwili ya nishati ya nyuklia ifikapo mwaka 2020.

Bychkov amesema tayari Belarus imetekeleza baadhi ya mapendekezo ya mwezi Juni na imepanga kutekeleza mapendekezo yaliyobakia, jambo linaloonyesha kuwa inachukulia ripoti hiyo kwa umakini.

Ripoti ya sasa ina mapendekezo 16 ya kuzingatiwa na serikali hiyo ili kuepusha madhara yoyote yanayoweza kutokea iwapo mradi wa nyuklia utaanza.

Mapendekezo hayo ni pamoja na kuangalia upya sheria za kudhibiti kuvuja kwa minururisho ya nyuklia, kuimarisha chombo kinachodhibiti nyuklia na kuendeleza mifumo bora ya usimamizi wa mradi wa nyuklia.

Harakati za Belarus kutaka kuwa na nishati ya nyuklia zilianza miaka ya 1980 na azimio rasmi lilipitishwa mwaka 2007.