Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wasyria milioni 26.5 wanahitaji msaada wa kibinadamu ndani na nje ya taifa lao:UN

Wanawake na watoto wa Syria waliotawanywa kutoka Mashariki mwa Aleppo wakipata hifadhi karibu na eneo la viwanda la al-Mahalij
UNHCR
Wanawake na watoto wa Syria waliotawanywa kutoka Mashariki mwa Aleppo wakipata hifadhi karibu na eneo la viwanda la al-Mahalij

Wasyria milioni 26.5 wanahitaji msaada wa kibinadamu ndani na nje ya taifa lao:UN

Amani na Usalama

Mgogoro wa Syria unaendelea kuwa changamoto kila uchao limesema shirika la Umoja wa Mataifa la misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA na kuongeza kuwa karibu watu milioni 26.5 wanahitaji msaada wa kibinamu ambapo milioni 14.6 wakiwa ndani ya Syria.

Hayo yameelezwa katika mkutano wa sita kuhusu Sytria unaomalizika leo mjini Brussels Ubelgiji wenye lengo la kusaidia mustakbali wa Syria na ukanda mzima.

Mkutano huo ambao umeandaliwa na Muungano wa Ulaya unatarajia kukamilika kwa ahadi za kulisaidia taifa hilo la Mashariki ya Kati na nchi za ukanda huo ambazo zimekuwa na ukarimu mkubwa wa kuhifadhi mamilioni ya wakimbizi kutoka Syria.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa watu wanaohitaji msaada ndani ya Syria idadi yao imeongezeka kwa watu milioni 1.2 tangu mwaka 2021 na takriban watu milioni 12 katika ukanda mzima wakiwmo watu milioni 5.6 ambao ni wakimbizi wa Syria na jamii zinazowahifadhi.

Dola bilioni 10 zahitajika kukidhi mahitaji

Kwa mwaka huu wa 2022 OCHA inasema kuna mikakati miwili mikubwa ya kukabiliana na mgogo wa Syria ambayo inahitaji dola bilioni 10.5 ambazo zitatumia kusaidia Wasyria na jamii zinazowahifadhi.

Na dola bilioni 4.4 zitawasaidia Wasyria walio ndani ya Syria huku zingine bilioni 6.1 ni za kusaidia wakimbizi na jamii zinazowahifadhi katika ukanda huo.

Wasichana vigori wakitumia simu za rununu na tablet katika kambi ya waki,mbizi ya Za'atari  inayohifadhi wakimbizi wa Syria.
© UNICEF/UN051302/Herwig
Wasichana vigori wakitumia simu za rununu na tablet katika kambi ya waki,mbizi ya Za'atari inayohifadhi wakimbizi wa Syria.

Hadi sasa maombi hayo ya fedha yamefadhiliwa kwa asilimia 8 na 11 mtawalia. Umoja wa Mataifa unasema zaidi ya asilimia 90 ya Wasyria wanaishi kwenye umasikini mkubwa huku masuala ya ukatili wa kijinsia na hatari kwa watoto vikiongezeka.

Na kutokana na vita vinavyoendelea hatari ya kuathiriwa na vifaa vya mlipuko na mambomu ya kutegwa ardhini ni kubwa. Mbali ya vita Syria inakabiliwa pian a changamoto kubwa ya kutokuwa na uhakika wa chakula ambapo watu milioni 12 wanalala njaa kila siku limesema shirika la OCHA.

Na kuhusu elimu takwimu zinaonyesha kuwa “mtoto mmoja kati ya wawili wa Syria hawasomi na wako katika hatari ya kutumbukia kwenye ajira za watoto, ndoa za utotoni, ndoa za shuruti, usafirishaji haramu wa binadamu na kuingiza jeshini na makundi yenye silaha.”

Ukarimu wa nchi jirani

Kwa mujibu wa mkuu wa OCHA Martin Griffith, mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR bwana Filippo Grandi na mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP bwana Achim Steiner nchi Jirani wa Syria za Uturuki, Lebanon, Jordan, Iraq na Misri zimekuwa wakarimu sana kwa kupokea na kuhifadhi mamilioni ya wakimbizi wa Syria na zinaendelea kufanya hivyo.

Hata hivyo viongozi hao wameuambia mkutano wa Brussels kwamba “shinikizo za kiuchumi na kijamii pia zinaongezeka kutokana na mzigo mkubwa wa wakimbizi.

Wameonhgeza kuwa jumuiya ya kimataifa imeonyesha ukarimu wake kwa miaka mingi na mengi yamefanikiwa katika kuwasia watu wa Syria lakini sasa uwekezaji wa kujikwamua ndani ya Syria unahitajika sanjari na msaada Zaidi wa kibinadamu.”

Wameoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kutowasahau Wasyria na madhila wanayopitia na kuwaomba wahisani kunyoosha mkono zaidi wa ahadi zao za msaada leo.