Guterres nchini Senegal: Vita vya Ukraine ni ‘Mgogoro mara tatu’ barani Afrika
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema vita nchini Ukraine vinazidisha "mgogoro mara tatu wa chakula, nishati na kifedha," kote barani Afrika.
Ameyasema hayo akiwa Dakar, mji mkuu wa nchi ya Senegal, katika ziara yake ya kwanza barani humo tangu kuanza kwa janga la COVID-19, Guterres amesema, “wakati wa mazungumzo ya hali ya kijamii na kiuchumi, haiwezekani kuto taja vita vya Ukraine na athari zake kwa Afrika.”
Katibu Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa ameyasema hayo baada ya kukutana na Rais wa Senegal Macky Sall, ambaye alisema kwamba vita vya Ukrainia ni “msiba wa kibinadamu” ambao unaweza kuwa na “athari kubwa kwa uchumi, hasa kwa nchi zinazoendelea.”
Mzozo wa Ukraine unaongeza bei ya chakula na mafuta duniani, Maafisa wakuu wa Umoja wa Mataifa wana wasiwasi kuwa kupanda kwa gharama kutawasukuma watu wengi zaidi kukumbwa na njaa na huenda kukasababisha kukosekana kwa utulivu wa kisiasa na machafuko ya kijamii katika baadhi ya maeneo ya Afrika, ambapo bei za vyakula zimeongezeka kwa theluthi moja tangu mwaka jana (2021).
Kabla ya uvamizi wa Urusi kuanza mnamo Februari 2022, mchanganyiko wa mabadiliko ya tabianchi, migogoro na janga la COVID-19, tayari ilikuwa inaathiri hali ya kijamii na kiuchumi barani Afrika, haswa katika eneo la Sahel ambalo linajumuisha Senegal.
Usawa wa chanjo na uhuru
Akiwa nchini Senegal kabla ya mkutano na waandishi wa habari Katibu Mkuu Guterres na Rais Sall walitembelea kituo kipya cha uzalishaji chanjo cha hali ya juu, ambacho kinajengwa na Institut Pasteur huko Dakar. Kituo hicho kitakapokamilika, kitaweza kutoa aina mbalimbali za chanjo ikijumuisha Pfizer-BioNTech, mojawapo ya chanjo zinazotumiwa sana dhidi ya COVID-19. Pia kitaweza kutengeneza chanjo za majaribio dhidi ya malaria na kifua kikuu.
Akizungumza mwishoni mwa Wiki ya Chanjo Duniani, Guterres alisema ni muhimu “kujenga usawa wa chanjo duniani kote,” na kwamba "haikubaliki" kwamba karibu asilimia 80 ya Waafrika hawajachanjwa dhidi ya COVID-19. ; hali ambayo aliiita “kutofaulu kwa maadili.”
Rais Macky Sall ametoa wito wa kuwepo kwa uhuru wa dawa kwa kusaidia kuibuka kwa tasnia ya dawa ya Kiafrika yenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya kimsingi na kukabiliana na milipuko.
Kama sehemu mojawapo ya mpango wa uokoaji wa COVID-19, Senegal inaimarisha sekta yake ya utengenezaji wa dawa. Inatarajiwa kuwa kituo cha chanjo kitazalisha angalau asilimia 50 ya mahitaji ya nchi.
Mwitikio wa mgogoro wa kimataifa
Ongezeko la uwekezaji ni sehemu ya mkakati wa kimataifa wa kusaidia nchi zinazoendelea zinazokabili kile ambacho Umoja wa Mataifa umekiita “migogoro inayoendelea.” Mnamo Machi 2022, Mkuu wa Umoja wa Mataifa alianzisha Kikundi cha Kukabiliana na Migogoro ya Ulimwenguni kuhusu Chakula, Nishati na Fedha (GCRG) kilianzishwa ili kukabiliana na mzozo uliochochewa na uvamizi wa Urusi kwa Ukraine, akisema kwamba uvamizi huo ulikuwa unaleta athari za kutisha kwa uchumi wa dunia ambao tayari umeathiriwa na COVID-19 na mabadiliko ya hali ya hewa.
Rais Macky Sall ni mmoja wa viongozi sita mashuhuri duniani ambao wametajwa kuwa Mabingwa wa kundi hilo na wanaounga mkono wito wa Katibu Mkuu wa kuchukua hatua za haraka kuzuia, kupunguza na kujibu mgogoro huo. Pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika kwa mwaka wa 2022.
GCRG, inatoa wito kwa nchi kutafuta njia bunifu za kufadhili ongezeko la mahitaji ya kibinadamu na ufufuaji wa maendeleo duniani kote na kutoa kwa ukarimu na mara moja fedha ambazo tayari zimeahidi.
Chakula, nishati na fedha
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dakar, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alisema “lazima tuhakikishe kuna mtiririko thabiti wa chakula na nishati katika masoko ya wazi, kuondoa vikwazo vyote visivyo vya lazima vya kuuza nje,” akiongeza kuwa "nchi lazima zipinge kishawishi cha kuhodhi na badala yake ziachilie akiba ya kimkakati ya nishati.”
Umoja wa Mataifa unakadiria kuwa robo ya watu bilioni wanaweza kuingizwa katika umaskini uliokithiri mwaka huu wa 2022 , unaosababishwa na matokeo ya mzozo wa Ukraine. Taasisi za fedha za kimataifa zina jukumu muhimu la kutekeleza na "lazima zitoe msamaha wa deni haraka kwa kuongeza ukwasi na nafasi ya kifedha," Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa alisema, “ili serikali ziepuke kushindwa na kuwekeza katika mitandao ya usalama wa kijamii na maendeleo endelevu kwa watu wao.”