Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu
Mtoto mwenye ulemavu wa ngozi tena mwenye ulemavu wa kutoona akisoma kwa kupitia maandishi maalum ua nukta nundu kwa watu wasioona au wenye uoni hafifu

Utafiti na Ushahidi juu ya Watoto wenye Ulemavu: UNICEF

© UNICEF/Pirozzi
Mtoto mwenye ulemavu wa ngozi tena mwenye ulemavu wa kutoona akisoma kwa kupitia maandishi maalum ua nukta nundu kwa watu wasioona au wenye uoni hafifu

Utafiti na Ushahidi juu ya Watoto wenye Ulemavu: UNICEF

Msaada wa Kibinadamu

Ingawa Malengo ya Maendeleo Endelevu yanahimiza kuwa hakuna mtoto anayepaswa kuachwa nyuma. Lakini utafiti uliofanywa na Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumiwa watototo UNICEF unaonesha kuwa kati ya watoto milioni 240 wenye ulemavu duniani, nusu hawajawahi kuhudhuria shule, takriban theluthi moja hawapati chakula bora na chakutosha na pia watoto wenye ulemavu wanawakilishwa kwa njia isiyo sawa na wengi wao wanaachwa nyuma. 

Nyuma ya takwimu hizo kuna hadithi nyingi za watoto, matarajio, na vikwazo watoto wenye ulemavu vinavyokabiliana navyo kila siku. 

UNICEF inadhamiria kuhakikishia kuna ujumuishaji wa watoto wote wenye ulemavu katika elimu, afya, majibu ya dharura, ulinzi wa kijamii, familia na maisha ya jamii.

Ni kutokana na dhamira hiyo, katika Mkutano wa Kimataifa wa Walemavu 2022, UNICEF inajitolea kutoa ushahidi mpya kupitia utafiti. Inajitolea kuanzisha Ajenda ya Utafiti wa Kimataifa na Jukwaa kwa watoto wenye ulemavu, na kuhakikisha wanajumuisha ulemavu katika utafiti zote, ili kuongeza uwekezaji katika ujumuishaji kwa watoto wote.

Kwa muda mefu UNICEF imekuwa ikifanya tafiti mbalimbali na hapa chini ni baadhi mifano ya utafiti na ushahidi wa miaka mitano iliyopita ambao unalenga watoto wenye ulemavu.

Mvulana wa Kipalestina mwenye umri wa miaka saba, ambaye ni kipofu, anatumia kifaa cha nukta nundu darasani, katika shule ya Hebron katika Ukingo wa Magharibi.
© UNICEF/Ahed Izhiman
Mvulana wa Kipalestina mwenye umri wa miaka saba, ambaye ni kipofu, anatumia kifaa cha nukta nundu darasani, katika shule ya Hebron katika Ukingo wa Magharibi.

Usaidizi wa Kiteknolojia 

Teknolojia ya usaidizi ifaayo ina athari chanya moja kwa moja kwa ustawi wa watoto kwa kusaidia kujishughulisha kwao na ushirikishwaji katika jamii, na hivyo kuongeza fursa za elimu, ajira na ushiriki wa kijamii. Kifupi usaidizi wa teknolojia ni kiwezeshaji kikuu cha kumuongezea mtoto uwezo wa kushiriki vitu. 
“Teknolojia za kusaidia kama vile viti vya magurudumu, vifaa bandia, visaidizi vya kusikia na miwani huwapa watu wenye ulemavu nafasi ya kushinda vizuizi na kuonesha kile wanachoweza kufanya badala ya kile wasichoweza.” Henrietta Fore Mkurugenzi Mkuu wa UNICEF

Mvulana mlemavu anaendelea na masomo wakati wa janga la COVID-19 huko Armenia.
© UNICEF/Grigoryan
Mvulana mlemavu anaendelea na masomo wakati wa janga la COVID-19 huko Armenia.


Janga la COVID-19

Janga la COVID-19 limeongeza hatari kwa watoto wenye ulemavu kwa sababu ya mahitaji yao makubwa ya uangalizi wa afya, utegemezi mkubwa kwenye huduma za jamii na maalum, ugumu wa kufuata mashariki ya umma kujikinga na maradhi, kupata vifaa vya kinga ya kibinafsi na ugumu wa kupata jumbe muhimu.

Namna ya kukabiliana na janga ilichochea uboreshaji katika ufikiaji wa elimu hata watu wakiwa mbali lakini haikuzingatia maswala ya ufikiaji kwa watoto wenye ulemavu.

“Covid-19 ilimaanisha usumbufu wa usaidizi wa masomo kwa watoto wenye ulemavu katika angalau asilimia 50 ya ulimwengu.”

Wanafunzi katika Kituo cha Kulelea watoto cha Quang Son katika Mkoa wa Ninh Thuan, Viet Nam. Kituo cha kulelea watoto mchana kinahudumia watoto wenye ulemavu, pamoja na watoto ambao ni wa makabila madogo katika eneo hilo.
UNICEF/Quan
Wanafunzi katika Kituo cha Kulelea watoto cha Quang Son katika Mkoa wa Ninh Thuan, Viet Nam. Kituo cha kulelea watoto mchana kinahudumia watoto wenye ulemavu, pamoja na watoto ambao ni wa makabila madogo katika eneo hilo.

Elimu shirikishi 

Elimu-jumuishi imekuwa ikikuzwa kimataifa kwa miaka mingi lakini mapungufu makubwa ya takwimu na ushahidi yameathiri upangaji, miundo na utekelezaji wa sera na mifumo ya elimu-jumuishi. Watoto wenye ulemavu mara nyingi hawaonekani na hukosa kuboresha fursa zao za masomo na maisha.

Mwanafunzi akiwa darasani kwake huko Paraguay, akijifunza kusoma na kuandika maandishi ya vipofu
© UNICEF/Brian Sokol
Mwanafunzi akiwa darasani kwake huko Paraguay, akijifunza kusoma na kuandika maandishi ya vipofu

Takwimu 

Takwimu juu ya watoto wenye ulemavu ni msingi wa utafiti kuhusu wao, kwao, pamoja nao. Bila takwimu hatuwezi kamwe kujua ukubwa au asili ya masuala. Kwa takwimu tuna uwezo wa kuelewa, kuchukua hatua, kuboresha, kujumuisha, kujenga msingi wa kujua ni nini kinachofaa kwa watoto wenye ulemavu.

UNICEF iko katika hatua ya kuanzishwa kwa kuanzisha Kituo mahususi cha Ubora wa takwimu kwa Watoto wenye ulemavu ili kuimarisha uwezo wa wadau kufanya maamuzi kwa wakati na yanayotokana na takwimu yanayohusu watoto wenye ulemavu.

“Kulinganisha na watoto wasio na ulemavu, watoto wenye ulemavu wana uwezekano mdogo wa kuwa na vitabu vya watoto kwa asilimia 57 na chini ya asilimia 32 wana uwezekano wa kutosoma kabisa vitabu au kutosoma vitabu nyumbani.”

Mwanafunzi mwenye ulemavu akiwa katika uwanja wa michezo nchini Brazil
© UNICEF Brazil
Mwanafunzi mwenye ulemavu akiwa katika uwanja wa michezo nchini Brazil

Unyanyapaa na ubaguzi 

Watoto wenye ulemavu wanashuhudia kutengwa katika kila nyanja ya maisha yao kwa sababu ya unyanyapaa na ubaguzi wa aina nyingi ikiwa ni pamoja na mawazo potofu, matarajio madogo, unyanyasaji, kutengwa, kuachwa, na kupigwa. 

Utafiti unachukua jukumu muhimu katika kutambua, kuelewa na kushughulikia mazoea changamano ya kijamii na kitamaduni na kanuni za kijamii zinazoathiri mitazamo hasi na tabia za kibaguzi zinazohitajika kukabiliwa ili kutokomeza unyanyapaa na ubaguzi.

Watoto waliotumikishwa kijeshi wakichora katika kituo cha UNICEF, Jamhuri ya Afrika ya Kati
UNICEF/Brian Sokol
Watoto waliotumikishwa kijeshi wakichora katika kituo cha UNICEF, Jamhuri ya Afrika ya Kati


Misaada ya kibinadamu

Kuna ushahidi mdogo kuhusu watoto wenye ulemavu katika maeneo yanayotoa misaada ya kibinadamu, hasa katika kupima na kuhakikisha kuondolewa kwa vikwazo na ufikiaji jumuishi wa programu na huduma za kibinadamu. 

Misaada ya kibinadamu inachangia zaidi ya nusu ya matumizi ya kila mwaka ya UNICEF, na inaendelea kuongezeka. Misaada hiyo inajumuishashughuli muhimu za kiutendaji na kisera kwa utafiti.