Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WHO yakataza mtu aliyepona COVID-19 kumchangia damu mgonjwa anayeugua COVID-19

Wafanyikazi wa Idara ya wagonjwa mahututi, Chuo Kikuu cha Matibabu cha Guangdong.
Department of Critical Care Medicine, Guangdong Medical University
Wafanyikazi wa Idara ya wagonjwa mahututi, Chuo Kikuu cha Matibabu cha Guangdong.

WHO yakataza mtu aliyepona COVID-19 kumchangia damu mgonjwa anayeugua COVID-19

Afya

Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO limewashauri wale wote waliougua COVID-19 na kupona kutochangia damu hususan wagonjwa wanaougua COVID-19 kwakuwa tafiti zinaonesha damu hiyo haimsaidii mgonjwa.

Ushauri huo umetolewa na WHO baada ya jopo lake la kimataifa la wataalamu wa miongozo kuchambua matokeo ya majaribio 16 yaliyohusisha wagonjwa 16,236 ambao wana maambukizi lakini hawako mahututi na wale wagonjwa wa COVID-19 walio mahututi.

Ingawa hatua za wali za utafiti huo zilionesha matumaini, lakini utafiti wa sasa  unaonesha dhahiri kuwa mtu aliyeugua na kupona COVID-19 akimuongezea damu mgonjwa anayeugua sasa COVID-19 haimsaidii kupata nafuu wala kupunguza uhitaji wake wakuwekwa kwenye mashine ya kusaidia kupumua na zaidi ya yote unaongeza gharama na kuchukua muda mrefu kumuwekea damu mgonjwa. 

Ni kutokana na ukweli huo ndio maaana WHO imepinga vikali matumizi ya damu kwa mtu aliyeugua na kupona kuwekewa wagonjwa wanaugua sasa wasio mahututi na wale walio mahututi, isipokuwa tuu damu hiyo inaweza kutumika katika muktadha wa kufanya majaribio yaliyodhibitiwa bila mpangilio kwakitaalamu ukifahamika kama RCT. 

Mmoja wa Raia wa Uganda akipokea chanjo yake ya kwanza ya Covid-19 huko Hoima, Uganda.
John Kibego
Mmoja wa Raia wa Uganda akipokea chanjo yake ya kwanza ya Covid-19 huko Hoima, Uganda.

 

Jopo la kimataifa la kutoa miongozo ni muhimu katika hali ambazo utafiti unatakiwa kufanyika haraka ili matokeo yake yawezekusaidia kwa mfano majanga yanayojitokeza kama COVID-19. Miongozo hii huruhusu watafiti kutoa matokeo mapya ya kazi zao walizotafiti awali na wataalamu wenzao kuzipitia na kutoa muhtasari kadri taarifa mpya zinapopatikana. 

Ili jopo kutoa mapendekezo yao, linazingatia mkusanyiko wa mambo kadhaa kama vile ushahidi unaotathmini manufaa na madhara yanayohusiana na utafiti, suala la maadili na mapendeleo, pamoja na kuangalia iwapo matokeo hayo yanauwezekano wa kutumika.