Nchi zaidi ya 20 kukabiliwa na njaa kali, hatua za haraka zahitajika kuepusha baa:WFP/FAO Ripoti

Ripoti mpya iliyotolewa leo na mashirika ya Umoja wa Mataifa imeonya kwamba katika nchi zaidi ya 20 duniani tatizo la njaa litaongezeka kwa kiasi kikubwa na kutoa wito wa hatua za haraka ili kuepusha janga kubwa zaidi na hatari ya baa la njaa.
Ripoti hiyo ya mashirika ya Umoja wa Mataifa lile la mpango wa chakula duniani WFP na la chakula na kilimo FAO iliyopewa jina “ maeneo yenye njaa” imesema katikia miezi ijayo bila msaada wa wa dharura haraka maisha ya mamilioni ya watu yatakuwa hatarini hasa nchini Yemen, Sudani Kusini na Kaskazini mwa Nigeria ambazo zinashika nafasi ya juu ya orodha hiyo zikikabiliwa na viwango vya juu vya njaa hivi sasa huku familia katika baadhi ya maeneo nchini Sudan Kusini na Yemen tayari ziko au zitakuwa hatarini kwa njaa kali na vifo.
Masshirika hayo yameongeza kuwa ingawa idadi kubwa yan chi zilizoathirika ziko Afrika , njaa kali inatarajiwa kuongezeka katika kanda nyingi duniani kuanzia Afghanistan barani Asia, Syria na Lebanon Mashariki ya Kati hadi Haiti Amerika ya Kusini na Caribbea.
Mashirika hayo yamesema zaidi ya watu milioni 34 ulimwenguni tayari wanakabiliwa na viwango vya dharura vya njaa kali, ikimaanisha kuwa ni hatua kidogo tu kuwa baa la njaa.
“Kiwango cha mateso kinatisha. Na ni jukumu letu sote kuchukua hatua sasa na kuchukua hatua haraka kuokoa maisha, kulinda maisha na kuzuia hali kuwa mbaya zaidi ", amesema Mkurugenzi Mkuu wa FAO Qu Dongyu.
“Katika kanda nyingi, msimu wa kupanda ndio umeanza tu au uko karibu kuanza. Lazima tukimbizane na wakati na tusiruhusu fursa hii ya kulinda, kuleta utulivu na hata kuongeza uzalishaji wa chakula wa ndani, kuteleza. ”
Kuna sababu kadhaa zinazochangia kuongezeka kwa ukosefu wa uhakika wa chakula, na mataifa yanakabiliwa na moja au mchanganyiko wa chachu muhimu ambayo ni pamoja na mizozo, janga la COVID-19, mabadiliko ya tabianchi na milipuko ya nzige.
Pia kuongezeka kwa changamoto za kuwafikia watu wenye mahitaji ya kibinadamu ni wasiwasi mwingine. “Tunashuhudia msiba ukitokea mbele ya macho yetu. Njaa inayochangiwa na mizozo, nakuchochewa na majanga ya hali ya mabadiliko ya tabianchi na janga la COVID-19 inabisha hodi kwenye mlangoni kwa mamilioni ya familia”, amesema David Beasley, Mkurugenzi Mtendaji wa WFP.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo Bwana Beasley ameongeza kuwa "Tunahitaji kwa dharura vitu vitatu ili kuzuia mamilioni ya watu kufa kwa njaa: Mosi, mapigano yanapaswa kukomeshwa, pili lazima turuhusiwe kufikia jamii zilizo katika mazingira magumu na kutoa msaada wa kuokoa maisha, na tatu zaidi ya yote tunahitaji wafadhili kuongeza dola bilioni 5.5 ambazo tunaziomba kwa ajili ya mwaka huu. ”
Fedha hizo zitatumika kwa msaada wa chakula cha kibinadamu, usaidizi wa kugawa pesa taslimu na hatua zingine za dharura za kusaidia kuokoa maisha, kulingana na ombi lililozinduliwa mapema mwezi huu na mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa.
Ripoti hiyo pia inapendekeza hatua muhimu katika kila "eneo lenye njaa" kushughulikia mahitaji ya sasa na ya baadaye, kama kuongeza chakula na msaada wa lishe, kutoa mbegu zinazostahimili ukame, kukarabati miundombinu ya uvunaji wa maji na kuanzisha miradi ya pesa-kwa-kazi.