Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Chonde chonde Uganda huu ni wakati wa kudhihirisha demekrasia yenu:UN 

Kuna wasiwasi kuhusu hali ya haki za binadamu Uganda kuelekea uchaguzi
Unsplash/Random Institute
Kuna wasiwasi kuhusu hali ya haki za binadamu Uganda kuelekea uchaguzi

Chonde chonde Uganda huu ni wakati wa kudhihirisha demekrasia yenu:UN 

Masuala ya UM

Wakati serikali na mamilioni ya wananchi wa Uganda wakijiandaa kushiriki uchaguzi mkuu wa Rais na wabunge unaotarajiwa kufanyika kesho Alhamisi Januari 14, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ametoa wito kwa wadau wote nchini humo kuhakikisha demokrasia inachukua mkondo. 

Kupitia taarifa iliyotolewa leo mjini New York Matrekani na msemaji wake, Katibu Mkuu Antoniuo Guterres amsema “Wadau wote wa kitaifa katika uchaguzi huu mnapaswa kuhakikisha kwamba upigaji kura unafanyika katika mazingira jumuishi, ya uwazi na kwa njia ya amani.” 

Taarifa hiyo imeongezsa kuwa Katibu Mkuu anatiwa hofu kufuatia riopoti za machafuko na hali ya mvutano inayoshuhudiwa katika sehemu za Uganda kabla ya upigaji kura hapo kesho na hivyo ametoa wito kwa wadau wote wa kisiasa na wafuasi wao kujizuia na matumizi yoyote ya kauli za chuki, vitisho na machafuko na kuhimiza kwamba “Madai na malalamiko yoyote ya uchaguzi yanapaswa kutatuliwa kupitia mfumo wa kisheria na kwa njia ya amani.” 

Bwana. Guterres ameitaka pia malaka ya Uganda hususan vikosi vya ulinzi kujizuia na matumizi ya nguvu katika kipindi hiki cha uchaguzi na kutekeleza wajibu wao kwa kuzingatia misingi iliyopo ya haki za binadamu. 

Pia Katibu Mkuu amerejelea ahadi ya Umoja wa Mataifa ya kusaidia juhudi za serikali ya Uganda za kuchagiza maendeleo endelevu SDGs na kujenga mustakabali bora kwa watu wake.