Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Taarifa potofu ziliongeza changamoto katika kukabili Corona

Mtu anarambaza kupitia mitandao ya kijamii.
World Bank/Simone D. McCourtie
Mtu anarambaza kupitia mitandao ya kijamii.

Taarifa potofu ziliongeza changamoto katika kukabili Corona

Afya

Umoja wa Mataifa na wadau wamezisihi nchi zote duniani kushughulikia kile walichoekelea kuwa ni janga la taarifa ambalo limeibuka kutokana na janga la ugonjwa wa Corona au COVID-19, katika ulimwengu wa kawaida na mtandaoni.

Janga hilo ni la kwanza katika historia ambapo teknolojia na mitandao ya kijamii imetumika kwa kuhabarisha watu na kuwaunganisha lakini vile vile kukandamiza harakati za kimataifa za kushughulikia janga hilo na hata kubinya kasi ya kudhibiti ugonjwa huo.

"Taarifa potofu zinagharimu masha. Bila taarifa sahihi, vifaa vya uchunguzi wa magonjwa havitumiki, kampeni za chanjo za kuokoa maisha haziwezi kufikia lengo lake na virusi vitaendelea kushamiri,” imesema taarifa ya wadau hao iliyotolewa leo Jumatano.

 “Tunasihi nchi wanachama ziunde na zisongeshe mipango ya utekelezaji ya kudhibiti janga la taarifa kwa kuhakikisha kuwa taarifa sahihi zinasambazwa kwa jamii na makundi yaliyo hatarini, taarifa ambazo zinazingatia sayansi na ushahidi, hali ambayo itaepusha kuenea kwa habari potofu, lakini wakati huo huo hatua hizo ziheshimu uhuru wa kujieleza." Wamesema wadau hao.

Serikali pia zimeombwa kuwezesha jamii ili ziweze kuandaa majawabu ya kukabilianana taarifa potofu.

Wadau kama vile vyombo vya habari na majukwaa ya mitandao ya kijamii yametakiwa kushirikiana na mfumo wa Umoja wa Mataifa, na kila upande uimarishe hatua zake za kusambaza taarifa sahihi ili kuzuia kuenea kwa taarifa za uongoz.

Mwanafunzi wa shule ya Sa.Francis ya Assisi akiwa na wasichana wenzake wakiangalia picha kwenye simu zao za rununu baada ya darasa katika mji wa Cebu katikati ya jimbo la Visayas Ufilipino
@UNICEF/Estey
Mwanafunzi wa shule ya Sa.Francis ya Assisi akiwa na wasichana wenzake wakiangalia picha kwenye simu zao za rununu baada ya darasa katika mji wa Cebu katikati ya jimbo la Visayas Ufilipino

Dharura ya mawasiliano

Taarifa hiyo iliyotiwa saini na Umoja wa Mataifa na mashirika yake 8 pamoja na shirikisho la  msalaba mwekundu duniain, IFRC, inafuatia mkutano kupitia mtandaoni ulioandaliwa na shirika la afya la Umoja wa Mataifa, WHO kando mwa mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Kupitia ujumbe wake wa video kwenye mkutano huo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres amesisitiza ni kwa vipi COVID-19 ni dharura ya mawasiliano.  “Punde tu baada ya virusi kusamba duniani kote, taarifa zisizo sahihi na potofu zilisambaa kupitia mitandao ya kijamii, na kuacha watu wakiwa wamechanganyiwa na hata kupata ushauri usio sahihi,” amesema Guterres.
 “Jawabu ni katika kuhakikisha kuwa taarifa zenye misingi ya kisayansi na miongozo ya kiafya inasambazwa haraka na kufikia watu popote pale walipo ambako wanahitaij taarifa.”

Sayansi, majawabu na mshikamano 

Wakati wa wote wa janga hla Corona, Katibu Mkuu amesisitiza umuhimu wa kukabili kusambaa kwa ushauri wa kiafya usio saihhi, kauli za chuki na fikra potofu zilizoibuka sambamba na COVID-19.

Mwezi Mei mwaka huu, Umoja wa Mataifa ulizindua mkakati wa uthibitishio, au Verified Initiative, ukihamasisha watu popote walipo duniani kuwa kama watoa usadizi wa kwanza ambao wanasambaza taarifa za kweli na sahihi kupitia majukwaa ya mitandao yao ya kijamii.

 

 “Kufanya kazi na wadau wa habari, watu binafsi, washawishi na majukwaa ya mitandao ya kijamii, taarifa tunazosambaza zinachochea sayansi, na zinatoa majawabu ambayo yanachochea mshikamano,” amesema Guterres.

Kama ambavyo Bwana Guterres ameelezea mkutano huo, kukabili taarifa potofu kutakuwa ni jukumu muhimu waktai huu ambapo Umoja wa Mataifa na wadau wake wanashirikiana kujenga imani ya umma kwenye usalama na ufanisi wa chanjo dhidi ya COVID-19 ambayo sasa inatengenezwa.

Kuendeleza kampeni za chanjo zilizositishwa

Ujumbe huo wa Katibu Mkuu ulipatiwa msisitizo wakati wa mkutano mwingine wa WHO uliofanyika kwa njia ya mtandao ukisihi serikali na wadau wa kibinadamu kulinda kampeni za chanjo wakati huu wa janga la Corona na kuhakikisha miundombinu iko ili itumike siku za usoni kusambaza chanjo dhidi ya COVID-19 ambayo bado inatengenezwa.

Ingawa Umoja wa Mataifa unakadiria kuwa takribani watoto milioni 80 kote duniani hawajapata chanjo za ratiba kutokana na janga  la Corona, WHO inasema kuwa huduma zinaanza kurejea kwa lengo la kuhakikisha wanaendelezea pale walipoachiwa.

Mkurugenzi wa Idara ya Utoaji wa Chanjo WHO, Karen O’Brien amesema wadau pia wanashirikiana kwa karibu zaidi kuwahi kutokea, na kwa mchangamano mkubwa ambapo kanuni wanazotumia zitatumika kusambaza chanjo dhidi ya Corona.

 “Lengo letu ni kuhakikisha kuwa chanjo inasambazwa kwa haki na kwa usawa kwa nchi zote, na kutumia ubia kushirikiana kuleta chanjo salama na nafuu. Na tufanye hivyo kwa sababu hakuna aliye salama hadi sote tuko salama,” amesema Bi. O’Brien.