Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Huduma ya afya haipaswi kuwa biashara bali haki ya binadamu:Byanyima 

Winnie Byanyima ambaye ni mkurugenzi mtendaji mpya wa UNAIDS akiwa kwenye moja ya mikutano ya kuwawezesha wanawake kiuchumi kwenye Umoja wa Mataifa.
UN Photo/Amanda Voisard
Winnie Byanyima ambaye ni mkurugenzi mtendaji mpya wa UNAIDS akiwa kwenye moja ya mikutano ya kuwawezesha wanawake kiuchumi kwenye Umoja wa Mataifa.

Huduma ya afya haipaswi kuwa biashara bali haki ya binadamu:Byanyima 

Afya

Mkurugenzi mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa linalopambana na ukimwi UNAIDS Winnie Byanyima amesema janga la corona au COVID-19 limeongeza adha kwa watu wanaoishi na VVU lakini pia kuyumbisha uchumi wa dunia na kuongeza pengo la usawa wa kijinsia, hivyo ameisihi dunia kuchukua hatua zinaozingatia haki za binadamu kama njia pekee ya kulidhibiti janga hilo.

Akizungumza mwishoni mwa wiki mjini Geneva katika kampeni ya kuhimiza kila mtu kusimama kwa ajili ya haki za binadamu ili kuhakikisha watu wasiojiweza na walio hatarini wanapata huduma za afya ikiwemo dawa za VVU na matibabu ya COVID-19  Bi. Byanyima amesema

“Tumejifunza katika hatua za kimataifa za kupambana na HIV kwamba mtazamo unaozingatia haki za binadamu wenye msingi wa kumthamini kila mtu kwa usawa unaweza kuvishinda virusi vya corona na vingine vitakavyokuja. Na hiyo ndio sababu nasimamia haki za binadamu na nasimama kwa ajili ya watu wote walio hatarini na wasio na sauti”

Akaenda mbali zaidi na kusisitiza kwamba huduma za afya kwa wote si suala la biashara bali ni haki anayostahili kila mtu

"Huduma za afya asilani hazipaswi kuwa bidhaa za kuuzwa, ni haki ya binadamu kwa wote na uwekezaji wa pamoja , kwa usalama wetu wote na ustawi. Ndio maana nasimama Pamoja na viongozi wa dunia katika madai yao ya chanjo yoyote au tiba itakayopatikana kwa ajili ya COVID-19, itangazwe kuwa ni kwa ajili ya jamii nzima na iweze kupatikana kwa nchi zote na kwa watu wote bure bila ghara yoyote.”