Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Vifaa na misaada kutoka kituo kikuu Addis Ababa vyaleta mabadiliko- WFP

Ndege ya mshikamano ya UN ikitokea Addis Ababa, Ethiopia itawasilisha vifaa tiba nchi kadhaa barani Afrika.
WFP/Edward Johnson
Ndege ya mshikamano ya UN ikitokea Addis Ababa, Ethiopia itawasilisha vifaa tiba nchi kadhaa barani Afrika.

Vifaa na misaada kutoka kituo kikuu Addis Ababa vyaleta mabadiliko- WFP

Msaada wa Kibinadamu

Shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa, WFP, limechukua hatua kuhakikisha kuwa wakati huu wa janga la ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19, vifaa vya matibabu pamoja na wafanyakazi wanaweza kufika popote pale wanapohitajika kwa wakati.

Shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa, WFP, limechukua hatua kuhakikisha kuwa wakati huu wa janga la ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19, vifaa vya matibabu pamoja na wafanyakazi wanaweza kufika popote pale wanapohitajika kwa wakati.

Hatua hiyo ni ni ile ya kuweka kwenye nchi zilizo hatarini zaidi au maeneo ya jirani shehena ya miezi mitatu ya chakula na vifaa vingine sambamba na kuhakikisha kuwa kuna fedha za kutosha kutekeleza mradi wa kupatia fedha wahitaji ili wakidhi mahitaij yao.

Ni katika misingi hiyo, uwanja wa ndege wa Bole mjini Addis Ababa nchini Ethiopia umeteuliwa na WFP kuwa kitovu cha safari zake ambapo vifaa vya kujikinga dhidi ya COVID-19 pamoja na dawa viliwasili kutoka Abu Dhabi, huku ndege nyingine ya mizigo ikiwa na aproni, barakoa, glovu, miwani ya kitabibu na vipima joto viliwasili Ethiopia tayari kusambazwa katika zaidi ya mataifa 30 ya Afrika.

Huko Norway nako, maandalizi ya vituo vya matibabu dhidi ya COVID-19 yanafanyika ambapo vikikamilika vituo hivyo vinasafirishwa kwenye mlipuko wa janga hilo kokote kule ulimwenguni.

Kwingineko nchini AFghanistani nako, wafanyakazi wa misaada wanachukua hatua za kujikinga dhidi ya COVID-19 kabla a kupanda ndege mjini Kabul tayari kwenda kutoa huduma.

Mkurugenzi wa WFP anayuhusika na uchukuaji hatua, Amer Daoudi anasema kuwa, “kiwango hiki cha operesheni katu hatujawahi shuhudia. Hii ni operesheni ya dunia iliyotandaa katika mataifa 120. WFP imepatiwa jukumu la kusimamia upelekaji wa vifaa vya matibabu na misaada ya kibinadamu. Ndio maana tumeanzisha hiki daraja hili la kianga la uokoaji maisha kutoka China, Ulana , Marekani na Mashariki ya Kati kwenda duniani kote.”

Nchini Somalia hususan katika mji mkuu Mogadishu, vifaa vya matibabu na vinginevyo kama vyakula vimewasili kwa ndege kutoka Ethiopia ambapo wafanyakazi wanapokea misaada na fedha na kusambaza kwa wananchi.

Miongoni mwa wanufaika wa mpango huo ni Hani Mohamed Abdikadir, mwenye umri wa miaka 21 na ana watoto watatu.

Hani anasema kuwa, “chakula ambacho tulikuwa tunapata kutoka madukani sasa kinaletwa nyumbani kwa gari. “Asante Mungu! Nina furaha sana. Imebadili mambo mengi kwenye maisha yangu kama vile kutuletea chakula nyumbani kama njia mojawapo ya kujikinga dhidi ya virusi vya Corona. Ninashukuru sana.”

WFP inasema kuwa hivi sasa ina mpango wa kuanzisha vituo vingine vya usafirishaji wa misaada ya kibinadamu huko Guangzhou, China, Liege, Ubelgiji, na Dubai, Falme za Kiarabu ambako bidhaa zinatengenezwa lakini inahitaji fedha.

Shirika hilo limesema hadi sasa limeomba fedha za nyongeza dola milioni 350 kusaidia operesheni hiyo lakni imepokea asilimia 24 pekee.