Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la Usalama lapitisha azimio kuidhinisha kuendelea kwa shughuli za operesheni za kibinadamu mpakani Syria

Umoja wa Mataifa umekuwa ukiwasilisha msaada wa kibinadamu kupitia mpakani kwa kipindi cha miaka sita.
OCHA/David Swanson
Umoja wa Mataifa umekuwa ukiwasilisha msaada wa kibinadamu kupitia mpakani kwa kipindi cha miaka sita.

Baraza la Usalama lapitisha azimio kuidhinisha kuendelea kwa shughuli za operesheni za kibinadamu mpakani Syria

Msaada wa Kibinadamu

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Ijumaa limepitisha azimio la kuongeza muda wa msaada wa kibinadamu mpakani na operesheni za kibinadamu Syria, lakini kwa kupitia mpaka na Uturuki tu.

Umoja wa Mataifa umekuwa ukiwasilisha misaada ya kibinadamu kwa kipindi cha miaka sita kupitia mpaka wa Syria ulitarajiwa kufikia ukomo wake Ijumaa jioni iwapo Baraza la Usalama lingekosa kuongeza muda kuendelea kufanya hivyo

Takriban wasyria milioni tatu hutegemea msaada ambao husafirishwa kutoka Uturuki, Iraq na Jordan.

Na kadri mahitaji ya kibinadamu yanavyoendelea kuongezeka katika jimbo la Idlib Kaskazini magharibi mwa Syria, msaada kupitia mpaka wa Uturuki ni muhimu.

Ongezeko la machafuko Kaskazini magharibi mwa Syria kumewafurusha watu 300,000 tangu Desemaba 12.

Kupitishwa kwa azimio

Pendekezo la azimio liliwasilishwa mbele ya Baraza la Usalama na Ujerumani na Ubelgiji na lilipitishwa kwa kura 11, huku nchi nne hazikupiga kura ikiwemo Urusi, China, Marekani na Uingereza ambao ni wanachama wa kudumu wa Umoja wa Matafa.

Kwa kupitishwa azimio hilo linaongeza muda wa operesheni za kibinadamu kwa kipindi cha miezi sita hadi Julai mwaka huu wa 2020. Msaada huo hautapitishwa Al-Ramtha na Al Yarubiyah ambayo ni mipaka iliyoko nchini Jordan na Iraq mtawalia.

Kupitishwa kwa misaada kupitia mipakani kumeidhinishwa kwa kipindi cha mwaka mmoja na Umoja wa Mataifa ukipitisha maeneo manne ya mpakani.

Azimio lililopitishwa linamuomba Katibu Mkuu kuripoti kwa Baraza la Usalma kufikia mwisho wa Februari 2020 kuhusu uwezekano wa kumia njia mbadala za kuvuka mpaka wa Al Yarubiyah kwa sababu ya kuhakikisha msaada ikiwemo msaada wa kiafya na vifaa tiba vinawafikia watu walio na mahitaji kote nchini kupitia njia za moja kwa moja na kuendana na muongozo wa misaada ya kibinadamu kwa kuzingatia utu,kutoegemea upande wowote na uhuru.

Mfumo wa kupitisha misaada mipakani na Umoja wa Mataifa kwa mara ya kwanza liidhinishwa mwaka 2014 kupitia azimio 2165 na jukumu lake lilikuwa limeongezewa muda kupitia azimio 2449 mwaka 2019 lakini lilitarajiwa kufikia ukomo wake Ijumaa jioni.

Iwapo azimio hilo halingepitishwa operesheni za Umoja wa Mataifa mpakani Syria zingesitishwa Ijumaa jioni.