Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa wataka uchunguzi huru Sudan.

Waandamanaji wakikusanyika mbele ya Makao Makuu ya jeshi la Sudan mjini Khartoum (11 April 2019)
Masarib/Ahmed Bahhar
Waandamanaji wakikusanyika mbele ya Makao Makuu ya jeshi la Sudan mjini Khartoum (11 April 2019)

Wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa wataka uchunguzi huru Sudan.

Haki za binadamu

Watalaamu wa Umoja wa Mataifa leo mjini Geneva Uswisi wameeleza wasiwasi wao mkubwa kuwa Sudan inaelekea katika shimo la ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu na hivyo wakalisihi baraza la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa kuanzisha uchunguzi huru kuhusu ukiukwaji waliofanyiwa wanaoandamana kwa amani tangu kuanza kwa mwaka huu.

Wataalamu walioteuliwa na baraza la haki za binadamu mjini Geneva wamenukuliwa wakisema, “kwa kiwango na uzito wa ukikukwaji wa haki za binadamu unaoripotiwa na uhitaji wa kuchukua hatua za haraka kuzuia kuongezeka kwa kasi, tunatoa wito kwa baraza na haki za binadamu kuanzisha uchunguzi ulio huru kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu nchini Sudan na kufuatilia kikamilifu hali inavyoendelea.”

Wataalamu hao wa Umoja wa Mataifa wameeleza kuhusu taarifa za kutisha kuhusu vifo na majeruhi tangu tarehe 3 mwezi Juni 2019 kutokana na matumizi ya nguvu kupita kiasi na vurugu zinazofanywa na vikosi vya serikali hususani kikosi cha RSF kinachopigana kwa niaba ya serikali dhidi ya waandamanaji.

“Moja ya majukumu muhimu ya nchi ni kulinda maisha. Katika operesheni za kutekeleza sheria, kutumia nguvu ambayo inaweza kugharimu maisha ya mtu, haikubaliki. Sheria za kimataifa zinawaruhusu maafisa usalama kutumia nguvu kubwa kama njia ya mwisho kabisa ili kujilinda wenyewe wanapokuwa katika hatari ya kujeruhiwa au kifo.” Wataalamu wamesema.

Wanawake wamekuwa katika mstari wa mbele katika maandamano ya amani nchini Sudan Kusini na wamekuwa miongoni mwa waathirika wa kwanza wa vurugu ikiwemo unyanyasaji wa kingono, wataalamu wamesema na kuongeza kuwa wanawake wengi wapigania haki za binadamu wamekuwa wakikamatwa kihorera kama nji ya kuwatisha. Wakati wengine wameachiwa, taarifa walizonazo wataalamu huru wa Umoja wa Mataifa ni kuwa wengine bado wako chini ya poilisi na wako katika mahitaji makubwa ya matibabu.

Vile vile wataalamu huru wamezitaka mamlaka nchini Sudan kufungua tena mtandao wa intaneti baada ya kuwa umefungwa tangu kuanza kwa mwezi huu wa Juni 2019.

Waandamanaji wamekuwa wakipigania mabadiliko ya kidemokrasia ikiwemo Baraza la mpito linaoundwa na jeshi, TMC kukabidhi madaraka kwa raia.

Baraza la usalama nalo latoa neno kuhusu hali ya Sudan

Wataalamu hao wanapopaza sauti zao, tayari jana baraza la usalama la Umoja wa Mataifa jana limetoa taarifa ya kulaani vikali vurugu hizo za hivi karibuni katika nchi hiyo ya jamhuri ya Sudan na wameeleza kusikitishwa kwao kutokana na vifo na majeruhi miongoni mwa raia. Wajumbe wa baraza hilo walieleza masikitiko yao na rambirambi kwa familia za waathirika na kuwatakiwa kupona haraka wale wote ambao wamejeruhiwa.

Wajumbe hao wa baraza walitaka kusitishwa haraka kwa unyanyasaji dhidi ya raia na wakasisitiza umuhimu wa kuheshimu haki za binadamu na kuhakikisha ulinzi kwa raia, kuwajibika na kufuatwa kwa haki.

Aidha baraza lilimuhamasisha Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuendelea na kuunga mkono juhudi za kikanda na kimataifa, hususani zile zinazoongozwa na muungano wa Afrika, kuratibu na kukubaliana kuhusu mchakato wa mpito wa kitafa kwa faida ya watu wa Sudan.