Huduma ya afya kwa wote ni haki si upendeleo- WHO
Leo ni siku ya afya duniani ambapo Umoja wa Mataifa unapatia mkazo suala la huduma ya afya kwa wote.
Mkurugenzi Mkuu wa shirika la afya ulimwenguni, WHO Dkt. Tedros Ghebreyesus amesema suala la huduma ya afya kwa wote ni lengo kuu la shirika hilo akisema hatua muhimu ya kufanikisha ni kuhakikisha kila mtu anapata huduma anayohitaji, pindi anapohitaji pale pale kwenye jamii yake.
Akizungumza mjini Geneva, Uswisi, Dkt. Ghebreyesus amesema ingawa kuna maendeleo yamefikiwa katika baadhi ya nchi za maeneo mbalimbali dunia kuona kila mtu anapata huduma ya afya, bado mamilioni ya watu wanalazimika kuchagua kati ya huduma ya afya na mlo, mavazi au hata makazi.
“Tupo hapa kuweka kauli thabiti kuwa afya ni haki na si upendeleo. Tupo hapa kusema kuwa watu wote wana haki ya kupata huduma ya afya wanayohitaji, pindi wanapotahiaji bila mkwamo wowote wa kifedha,” amesema Mkurugenzi Mkuu huyo wa WHO wakati wa tukio maalum lililofanyika mjini Geneva.
Amesema WHO ndio mwamba wa huduma ya afya ya msingi kwa wote na kwamba, “huduma ya afya ya msingi kwa wote inahusisha mahitaji yote makubwa ya afya ya binadamu. Inasaidia pia kuepusha watu kwenda hospitali na kusalia kwenye jamii zao.”
Kwa mantiki hiyo amesema katika siku ya afya duniani mwaka huu wa 2019, wanatoa wito kwa mataifa kuwekeza katika huduma za msingi za afya.
Amekumbusha kuwa maadhimisho ya mwaka huu ya siku ya afya duniani, yanafanyika katikati ya mkutano wa afya kwa wote uliofanyika Astana, Kazakhstan mwezi Oktoba mwaka jana na kikao cha ngazi ya juu kuhusu afya kwa wote kitakachofanyika wakati wa mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani mwezi Septemba mwaka huu wa 2019.
|