Elimu maalum Sudan Kusini bado ni changamoto- UNICEF
Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, limetaka wadau wa elimu nchini Sudan Kusini kuongeza juhudi ili kuhakikisha watoto wenye ulemavu wanaandikishwa shuleni.
Mkuu wa masuala ya elimu, UNICEF Mokhtar Shirin, akihojiwa na radio Miraya ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini, UNMISS kuwa hali si nzuri kwa watoto hao kwasababu kuna mtazamo hasi dhidi ya elimu hususan kwa watoto wa kike na wale wenye mahitaji ya maalum.
Halikadhalika amesema kuna uhaba rasilimali, walimu wenye mafunzo mahsusi kwa ajili ya elimu maalum sambamba na mizozo inayoendelea ambayo inakwamisha watoto kwenda shuleni kujifunza.
Hata hivyo Bi. Shirin amesema.
“Wizara imetunga sera kusaidia watoto wenye mahitaji maalum na UNICEF tunaendelea kushirikiana na wizara kuhakikisha kuwa hili linatekelezwa. Mfano shule zilizojengwa chini ya usaidizi wa kamisheni ya kimataifa ya elimu zinakuwa na miundombinu ya ujumuishi zikifikiria pia watoto wenye ulemavu ambapo zinakuwa na njia maalum za kwenda darasani na maeneo mengine.”
Bi. Shirin ametaja pia suala la mishahara isiyotosha ya walimu akisema wanahitaji motisha na hivyo suala la msingi ni kuongeza bajeti ya elimu kama njia mojawapo ya kusaidia watoto wenye mahitaji walimu.