Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wimbi kubwa la Tsunami laleta madhara makubwa Indonesia, UN yasema iko tayari kusaidia

Madhara ya Tsunami na tetemeko Indonesia yaliwaacha wengi bila makazi.
UNICEF/Arimacs Wilander
Madhara ya Tsunami na tetemeko Indonesia yaliwaacha wengi bila makazi.

Wimbi kubwa la Tsunami laleta madhara makubwa Indonesia, UN yasema iko tayari kusaidia

Msaada wa Kibinadamu

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameeleza masikitiko yake makubwa kufuatia vifo, majeruhi na uharibifu mkubwa uliosababishwa na wimbi kubwa la tsunami lililopiga maeneo  ya pwani ya kisiwa cha Sumatra nchini Indonesia jana Jumamosi.

Katika taarifa iliyotolewa na msemaji wake mjini New York, Marekani leo Jumapili, Bwana Guterres ametuma salamu za rambirambi kwa familia za waliofariki dunia pamoja na serikali ya Indonesia huku akiwatakia ahueni ya haraka majeruhi.
 
Halikadhalika, Katibu Mkuu amesema, “Umoja wa Mataifa uko tayari kusaidia juhudi zinazondelea za uokoaji zinazofanywa na serikali ya Indonesia.”
 
Vyombo vya habari vinaripoti kuwa takribani watu 200 wamefariki dunia na zaidi ya 850 wamejeruhiwa baada ya wimbi hilo la tsunami kupiga miji ya pwani ya Sunda kwenye kisiwa cha Sumatra.
 
Hadi sasa watu kadhaa hawajulikani walipo huku barabara za kawaida za magari pamoja na barabara kuu zikiwa zimeharibiwa.


Tafadhali iwapo unataka kupokea taarifa kutoka UN News Kiswahili kila wakati zinapochapishwa, tafadhali jisajili na pia unaweza kupakua apu ili kuweza kusikiliza wakati wowote popote ulipo.