Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mnaohasimiana Sudan Kusini heshimuni makubaliano kati yenu- UN

Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa UN nchini Sudan Kusini, David Shearer akizungumza na waandishi wa habari mjini Juba hii leo tarehe 19 septemba 2018 kuhusu utekelezaji wa makubaliano  kati ya pande kinzani kwenye mzozo nchini humo.
UNMISS/Isaac Billy
Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa UN nchini Sudan Kusini, David Shearer akizungumza na waandishi wa habari mjini Juba hii leo tarehe 19 septemba 2018 kuhusu utekelezaji wa makubaliano kati ya pande kinzani kwenye mzozo nchini humo.

Mnaohasimiana Sudan Kusini heshimuni makubaliano kati yenu- UN

Amani na Usalama

Umoja wa Mataifa umezitaka pande kinzani nchini Sudan Kusini ziheshimu makubaliano mapya ya kusitisha mapigano ambayo pande hizo zilitia saini hivi karibuni ili kumaliza mapigano yaliyogubika nchi hiyo tangu mwezi disemba mwaka 2013. Assumpta Massoi na ripoti kamili.

Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa MAtaifa nchini Sudan Kusini, David Shearer, amesema hayo leo kwenye mji mkuu Juba wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alikuwa akigusia makubaliano  hayo ya kusitisha mapigaon yaliyotiwa saini kati ya Rais Salva Kiir na makamu wake wa zamani wa rais Riek Machar akisema Umoja wa Mataifa  unataka kuona ushahidi bayana kuwa pande zote zina utashi wa kisiasa kukomesha ghasia. Hata hivyo amesema..

(Sauti ya David Shearer)

“ Kwa sasa kuna kiungo muhimu kinachokosekana,  nacho ni kuaminiana. Waliotia saini katika makubaliano hayo  zamani walikuwa marafiki na kisha wakageuka kuwa maadui . Kutokana na mazungumzo yangu nao bado kila upande unaushuku mwingine. Kwa hivyo inahitajika kufanya kazi kubwa waweze kuaminiana kati yao na pia na kati ya pande hizo na watu wa Sudan Kusini. Na tunahitaji kushirikiana kwa hilo.”

Walinda amani wa UN wakiwa katika doria huko juba Sudan Kusini.
UNMISS
Walinda amani wa UN wakiwa katika doria huko juba Sudan Kusini.

Kwa mantiki hiyo Bwana Sheare ambaye pia ni mkuu wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini, UNMISS amesema..

(Sauti ya David Shearer)

“Umoja wa Mataifa  uko tayari kusaidia utekelezaji wa makubaliano hayo, lakini lazima kuwepo na ratiba ya utekelezaji inayokubalika na pande zote kuweza kufikia hilo.”

Amezikumbusha pande zote husika kwenye makubaliano hayo kuwa mkataba ulitaka mapigano  yasitishwe ndani ya saa 72 tangu kutiwa saini, lakini hadi sasa ingawa kiwango cha mapigano kimepungua bado kuna ripoti za mapigano ya hapa na pale.