Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mzigo wa wakimbizi wa Rohingya ni jukumu letu sote:Guterres

Msichana mkimbizi akiwa amesimama nje kwenye nvua katika kambai ya Shamlapur, Cox's Bazaar
UNHCR/Patrick Brown
Msichana mkimbizi akiwa amesimama nje kwenye nvua katika kambai ya Shamlapur, Cox's Bazaar

Mzigo wa wakimbizi wa Rohingya ni jukumu letu sote:Guterres

Wahamiaji na Wakimbizi

Mzingo wa zahma ya wakimbizi wa Rohingya sio jukumu la serikali ya Bangladesh pekee bali unapaswa kuwa ni jukumu la dunia nzima. Wito huo umetolewa leo na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kwenye kikao cha Baraza la Usalama kuhusu hali ya wakimbizi wa Rohingya, kilichofanyika kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York Marekani.

 

Guterres amesema zahma hiyo iliyoanza mwaka mmoja uliopita jimboni Rakhine nchini Myanmar sasa imekuwa moja ya majanga makubwa kabisa ya kibinadamu na haki za binadamu duniani.

 

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres akihutubia Baraza la Usalma kikao juu ya Myanmar. Ikiwa ni mwaka mmoja tangu janga la Rohingya mwaka 2017.
UN Photo/Evan Schneider
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres akihutubia Baraza la Usalma kikao juu ya Myanmar. Ikiwa ni mwaka mmoja tangu janga la Rohingya mwaka 2017.

Ameongeza kuwa pamoja na juhudi kubwa alizozifanya ikiwa ni pamoja na kuzungumza na mamlaka ya Myanmar, miradi mbalimbali ya Umoja wa Mataifa kwa wakimbizi hao, kuteua mjumbe maalumu wa kwa ajili ya Myanmar na hata juhudi za mashirika ya Umoja wa Mataifa kama lile la kuhudumia wakimbizi UNHCR  na lile la maendeleo UNDP kukamilisha makubaliano na serikali ya Myanmar ya kuanzisha mkakati wa ushirikiano wa kuweka mazingira mazuri kwa wakimbizi kurejea nyumbani kwa hiyari , usalama na hali ya kiutu, bado kuna changamoto

(SAUTI YA ANTONIO GUTERRES)

“Bila shaka yote haya yanahitaji uwekezaji mkubwa sio tu katika ujenzi na maendeleo kwa jamii zote katika moja ya majimbo masikini kabisa nchini Myanmar, lakini pia katika upatanishi na kuheshimu haki za binadamu.”

Maelfu ya wakimbizi wa Rohingya wapanga msururu wa kupata chakula katika kituocha wakimbizi cha balukhali, Cox's Bazar.
UNICEF/Patrick Brown
Maelfu ya wakimbizi wa Rohingya wapanga msururu wa kupata chakula katika kituocha wakimbizi cha balukhali, Cox's Bazar.

Amesisitiza kuwa juhudi zaidi zinahitaji kufanywa ili kuondoa hatari inayokabili maisha ya watu. Hata hivyo ameishukuru Benki ya Dunia na Benki ya maendeleo barani Asia kwa mchango wao wa mamilioni ya dola ambao amesema ni muhimu sana ingawa ameongeza kuwa

(SAUTI YA ANTONIO GUTERRES )

“Bado wakimbizi wanahitaji fursa zaidi za elimu na maisha ili kuepuka hatari ya usafirishaji haramu wa binadamu, kunyanyaswa kingono na kuingizwa katika idikadi Kali.”

 Na katika kuponya majeraha ya jamii ya Rohingya amehimiza

(SAUTI YA ANTONIO GUTERRES )

“ Ni wajibu wa viongozi wa serikali ya Myanmar kuonyesha nia kwa kuzingatia misingi ya usawa na kutofanya ubaguzi na kupambana na vitendo vinavyochochea chuki kwa misingi ya ubaguzi wa rangi na ghasia, uwajibikaji ni muhimu kwa maridhiano ya kweli baina ya makundi yote ya kijamii na ni chachu ya usalama na utulivu kwa kanda nzima”

 Lakini kinachomsikitisha zaidi Guterres amesema ni serikali ya Myanmar kukataa kutoa ushirikiano vyombo vya haki za vinadamu vya Umoja wa Mataifa licha ya wito unaotolewa mara kadhaa wa kuitaka ifanye hivyo ukiwemo ule wa wajumbe wa Baraza la usalama.

 

Cate Blanchett, balozi mwema wa  Shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR akihutubia Baraza la Usalama juu ya Myanmar.
UN Photo/Manuel Elías
Cate Blanchett, balozi mwema wa Shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR akihutubia Baraza la Usalama juu ya Myanmar.

Amesema ushirikiano wa kimataifa wenye ufanisi utakuwa muhimu kwa kuhakikisha kuwa utaratibu wa uwajibikaji ni wa kuaminika, wa uwazi, usio na upendeleo, unaojitegemea na unaozingatia wajibu wa Myanmar chini ya sheria za kimataifa.

Naye balozi mwema wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR,  Kate Blanchet ambaye alizuru Myanmar kujionea hali halisi akizungumza kwenye kikao hicho cha Baraza la Usalama amesema maelfu ya wanawake wa Rohingya na watoto wao wanendelea kuishi na majinamizi na kuhimiza mshikamano wa kila mtu kusaidia zahma ya Rohingya kwani

(SAUTI YA CATE BLANCHET)

“Wengi wao bado wanakabiliana na makovu ya madhila na majeraha waliyoyapata kabla na wakati wa kukimbilia Bangladesh.Ni muhimu sana kwa serikali, mashirikya ya maendeleo na ya kibinadamu, sekta binafsi na watu binafsi kushikamana kutafuta njia bunifu za kuwasaidia wakimbizi na jamii za Bangladesh zinazowahifadhi.”