Maafisa wa jeshi Myanmar lazima washitakiwe kwa mauaji ya kimbari: UN ripoti
Maafisa wakuu wa jeshi nchini Myanmar, ikiwa ni pamoja na kamanda Mkuu Min Aung Hlaing, wanapaswa kuchunguzwa na kushtakiwa kwa mauaji ya kimbari, uhalifu dhidi ya binadamu na uhalifu wa vita, kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa leo mjini Geneva Uswisi na jopo huru la kiamtaifa la uchunguzi dhidi ya Myanmar.
Jopo hilo lililoundwa Machi 2017 na baraza la haki za binadamu limebaini kwamba kumekuwa na mwenendo wa ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu na ukatili kwenye majimbo ya Rakhine, Kachin na Shan na bila shaka limesema vitendo hivyo ni uhalifu mkubwa na mbaya zaidi chini ya sheria za kimataifa ambao kimsingi umetekelezwa na jeshi la Myanmar lijulikanalo kama “Tatmadaw’ lakini pia na vikosi vingine vya uslama. Christopher Sidoti ni mmoja wa wajumbe wa jopo hilo huru
“Jopo hili limehitimisha kuwa uchunguzi wa uhalifu na mashtaka ni lazima, vikiwalenga wakuu wa Tatmadaw kwa kuhusiana na aina tatu za uhalifu chini ya sheria za kimataifa; mauaji ya kimbari, uhalifu dhidi ya ubinadamu na uhalifu wa vita.”
Uhalifu huo uliotekelezwa katika majimbo hayo matatu ni pamoja na mauaji, watu kufungwa, watu kutoweshwa, utesaji, ubakaji, utumwa wa kingono na mifumo mingine ya ukatili, zaidi ya hayo kwenye jimbo la Rakhine ukatili mwingine dhidi ya ubinadamu iluobainika ni kuangamiza na kufurusha watu kwa lazima.
Radhika Coomaraswamy, ni mjumbe mwingine katika jopo hilo
"kiwango cha ukatili, na utaratibu wa ubakaji na unyanyasaji unaonyesha kuwa ni sehemu ya mkakati wa makusudi wa kutishia, kuogofya, au kuwaadhibu raia. Tumebaini wamevitumia videndo hivyo kama mbinu ya vita ikiwa ni pamoja na ubakaji, ubakaji wa kikundi, utumwa wa ngono, udhalilishaji wa kulazimishwa, na kuchinjwa. "
Kwa mantiki hiyo mwenyekiti wa jopo hilo Marzuki Darusman amesema
"Jopo hili linataka hali hiyo ya Myanmar ipelekwe kwenye mahakama ya kimataifa ya jinai na kwamba, bila shaka ni kazi ya Baraza la Usalama kufanya hivyo. Kwa hiyo, ujumbe kwa Baraza la Usalama ni kwamba, ipeleke Myanmar kwa ICC, kwa kuzingatia kuwa sasa uwajibikaji hauwezi kufanyika ndani ya Myanmar, msukumo lazima uje kutoka jumuiya ya kimataifa."
Maelfu kwa maelfu ya raia wa Myanmar walilazimika kufungasha virago baada ya machafuko yaliyozuka Agosti 25 mwaka 2017 kufuatia kundi lenye silaha la ARSA kufanya mashambulizi dhidi ya vituo vya jeshi na vikosi vya uslama kwenye jimbo la Rakhine na jeshi kujibu mashambulizi hayo kwa nguvu kupita kiasi na kusababisha mauaji na uharibifu mkubwa ukiwemo kuteketezwa kwa moto makazi ya Warohingya.