Wasifu wa Kofi Annan
Kofi Annan, raia wa Ghana ambaye alikuwa Katibu Mkuu wa 7 Umoja wa Mataifa kutoka mwaka 1997 hadi 2006.
AJIRA
Bw Annan alijiunga na Umoja wa Mataifa mwaka 1962 kama afisa wa utawala pamoja na masuala ya bajeti kwenye shirika la afya duniani WHO mjini Geneva.
Baadaye alifanya kazi kwenye mashirika na ofisi mbalimbali za Umoja wa Mataifa ikiwemo tume ya kiuchumi ya Afrika mjini Addis Ababa, Ethiopia, na na pia katika shirika la kuwahudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR mjini Geneva.
Aliteuliwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa tarehe 13 mwezi disemba mwaka 1996 kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na hatimaye kuidhinishwa na Baraza Kuu na kisha kuanza kutekeleza jukumu hilo tarehe 1 Januari mwaka 1997.
MCHANGO WAKE UNAOKUMBUKWA
Jambo kubwa alilotilia maanani wakati wa uongozi wake ni marekebisho ya muundo wa Umoja wa Mataifa kwa lengo la kufanya chombo hicho kilichoanzishwa mwaka 1945 kuwa na ufanisi zaidi.
Wavuti wa Umoja wa Mataifa kuhusu wasifu wa Makatibu Wakuu unasema kuwa alikuwa mchechemuzi asiyechoka wa haki za binadamu, utawala wa sheria, malengo ya maendeleo ya milenia na bara la Afrika akilenga kusaka ukaribu wa Umoja wa Mataifa na umma wa dunia kwa kuleta karibu mashirika ya kiraia, sekta binafsi na wadau wengine.
Enzi za uongozi wake, operesheni za ulinzi wa amani za Umoja wa Mataifa ziliimarishwa kwa njia iliyowezesha chombo hicho kwenda sambamba na ongezeko la operesheni na watendaji.
Mwaka 1998 aliwezesha kipindi cha mpito cha kurejesha utawala wa kiraia nchini Nigeria, halikadhalika mkwamo kati ya Umoja wa Mataifa na serikali ya Iraq.
KUZALIWA
Bw Annan alizaliwa Kumasi , Ghana , tarehe 8 Aprili mwaka 1938 na alikuwa na umahiri mkubwa wa kuzungumza lugha kadhaa ikiwemo Kiingereza, Kifaransa na lugha zingine za Kiafrika. Ameacha mjane aitwae Nane na watoto watatu.
Elimu
Bw Annan alisomea Chuo Kikuu cha sayansi na teknolojia cha Kumasi Ghana na kuhitimishia shahada yake ya kwanza ya uchumi katika Chuo cha Macalester jimboni Minnesota nchini Marekani mwaka1961. Alichukua masomo ya masuala ya kimataifa Geneva Uswisi kutoka mwaka wa 1961 hadi 1962 na mwaka wa 1972 alipata shahada ya uzamili katika taasisi ya teknolojia ya Massachusetts nchini Marekani, MIT.
Tuzo
Bwana Annan pamoja na Umoja wa Mataifa walipatiwa tuzo ya amani ya Nobel mwaka 2001 kutokana na mchango wake wa kusaka haki za binadamu duniani.