Dkt. Mukwege na Nadia Murad washinda tuzo ya amani ya Nobel
Tuzo ya amani ya Nobel yatangazwa hii leo huko Oslo Norway! Hafla ya kukabidhi tuzo kufanyika tarehe 10 mwezi huu. Na washindi ni balozi mwema wa UNODC Nadia Murad na Dkt. Denis Mukwege bingwa wa masuala ya wanawake kutoka DRC.
Nadia Murad, mwanaharakati kutoka kabila la Yazid nchini Iraq na balozi mwema wa kwanza wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kudhibiti madawa na uhalifu UNODC kwa ajili ya utu wa manusura wa usafirishaji haramu wa binadamu, na Daktari bingwa wa masuala ya wanawake, Dkt. Denis Mukwege anayesaidia waathirika wa ukatili wa kingono nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC, leo wametangazwa washindi tuzo ya amani ya Nobel ya mwaka 2018.
Umoja wa Mataifa umesema uamuzi wa kuwatunukia tuzo ya amani ya Nobel ya mwaka huu kwa pamoja Nadia Murad na Dkt. Mukwege utasaidia kukomesha matumizi ya ukatili wa kingono kama silaha ya vita.
Akikaribisha tangazo hilo lililotolewa Norway kwa niaba ya Umoja wa Mataifa mjini Geneva Uswis , msemaji wa Umoja huo Alessandra Velluci amesema kukomesha ukatili wa kingono katika migogoro ya vita inasalia kuwa kipaumbele cha Umoja wa Mataifa.
Ameongeza kuwa anakumbuka hili ni suala linalopigiwa upatu sana na Umoja wa Mataifa na hata kuna mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu ukatili wa kingono katika maeneo ya vita , Pramila Patten na kuongeza “nina uhakika tuzo hii itasaidia kusongesha harakati za kutokomeza ukatili wa kingono kutumika kama silaha ya vita na pongezi kubwa kwa washindi.”
Tangazo hilo pia limekaribishwa na ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kudhibiti madawa na uhalifu UNODC ambayo ilimteua mwaka 2016 Bi. Murad kuwa balozi mwema kwa ajili ya utu wa waathirika wa usafirishaji haramu wa binadamu kutokana na madhila aliyokabiliana nayo mikononi mwa kundi la kigaidi la ISIL nchini Iraq.
Mkurugenzi mkuu wa UNODC Yury Fedotov amempongeza Murad na kusema “Anatukumbusha kwamba ni lazima kila wakati kuwasikiliza watu ambao wameathirika na kuumizwa na uhalifu ambao tunataka kuutokomeza na shuhuda za manusura kama Bi. Murad ni lazima ziimarishe juhudi zetu na kuhakikisha haki inatendeka.”
Naye Dkt. Mukwege ambaye amepatiwa jina na vyombo vya habari kama “Mtu anayewarejesha hadhi yao wanawake” amejinyakulia umashuhuri mkubwa kimataifa kwa kazi yake na kushinda tuzo mbalimbali ikiwemo tuzo ya Umoja wa Mataifa ya Haki za binadamu mashinani 2008 na tuzo ya Sakharov mwaka 2014. Hata hivyo kaze yake imekuwa ikimsababishia changamoto kubwa , akihojiwa na idhaa hii mwaka 2014 alisema pamoja na mtihani unaomkabili na vitisho dhidi ya maisha yake kazi hii ni wito wake na hawezi kuiacha
(SAUTI YA DKT DENNIS MUKWEGE )
Na moja ya changamoto kubwa katika utendaji wake amesema
(SAUTI YA DKT DENNIS MUKWEGE )
Dkt. Mukwege ambaye ametibu maelfu ya wanawake waliobakwa katika hospitali ya Pazi nchini DRC ameshaingia mara nyingi kwenye orodha ya mchujo ya wanaowania tuzo hiyo ya Nobel na safari hii akaibuka kidedea.
.