Urusi yasema katu isihusishwe na kilichotokea Douma
Kufuatia madai ya matumizi ya silaha za kemikali huko Douma nchini Syria, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limekutana kujadili suala hilo ambapo Umoja wa Mataifa unaelezea masikitiko yake huku Urusi ikikanusha kuhusika kwa njia yoyote ile.
Akizungumza kwenye mkutano huo mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu Syria, Staffan de Mistura amesema ameshtushwa na kinachoendelea nchini Syria, akionya juu ya hatari za kuongezeka kwa kasi ya matatizo ambayo inaweza kuwa na matokeo mabaya na magumu kufikirika.
Mwakilishi wa kudumu Marekani katika Umoja wa Mataifa Balozi Niki Hailey ameendelea kulaani serikali ya Syria akidai inahusika na matumizi ya silaha za kemikali huku ikiungwa mkono na Urusi na Iran katika mgogoro huo ambao umechukua zaidi ya miaka 7 na kusabaisha vifo vya maelfu ya wa Syria na ukimbizi wa mamilioni ya wa Syria.
Akijibu tuhuma hizo, Balozi Vasily Nebenzya ambaye ni mwakilishi wa kudumu wa Urusi kwenye Umoja wa Mataifa amekanusha madai hayo akisema ni kampeni inayofanywa na nchi za magharibi ikiwa ni njama za kuichafua nchi yake.
Kikao hicho cha dharura cha Baraza la Usalama kiliitishwa na Urusi, Kuwait na Bwana de Mistura.